Mukwava inasemekana alizaliwa Luhota kwenye mwaka 1855.
Alipokuwa mdogo aliitwa Ntasalatsi, yaani mtu mwenye kupapasa kwa mikono na
vidole anapotafuta kitu. Mkwava aliishi kwenye nyumba iliyokuwa haikosi
simulizi za ushujaa wa baba yake na askari wake. Akiwa bado mdogo baba yake, Mutwa Munyigumba, alikwenda kuwa kuwapiga Wasangu na kupanua utawala wake mpaka Ng’uluhe.
Mutwa Mihwela alipokufa, mtawala ambaye alikuwa mjomba wa Muyingumba na aliwahi kumlea kwa muda mrefu, Muyigumba alifanya kila hila
mpaka binamu yake Myovela akalazimika kukimbia himaya yake na kwenda kujificha
Ugogoni, na Munyigumba aliweza kuiteka kirahisi himaya hiyo na ikawa chini
yake, na baadae akaweza kumnyan'ganya himaya binamu yake mwingine Mwengamagoha,
mdogo wake Myovela, ambaye naye alilazimika kukimbilia alikokuwa kaka yake. Munyigumba
akaweza kuunganisha koo ndogondogo nyingi kuwa chini yake na hakika alikuwa ni
muhimili mwingine katika ujenzi wa kabila la Wahehe.
Munyigumba akaweka
Ivaha(ikulu) yake Muhana sehemu
iliyoka jirani na Luhota, na huko ndiko kulikuwa na kambi ya kuwazoesha vijana
wa jeshi lake mbinu za vita. Kwa vile utawala wake ulipanuka sana, Munyigumba
akaweka watu wake waaminifu kuwa viongozi kwenye sehemu mbalimbali alizokuwa
akizitawala. Viongozi hawa waliitwa Vanzagila. Hawa pia walikuwa viongozi wa
jeshi lililokuwa chini yao ambalo Mutwa angeweza kuwaita wakati wowote.
Kati ya mateka wa vita za Muyigumba alikuweko mateka mmoja
wa Kinyamwezi, mateka huyu alikuwa mtoto. Mateka huyu alianza kutumiwa kwa
kutumwa kubeba dawa za zilizoaminika kuwa ndizo zilikuwa za kulinda ukubwa, akaanza kuaminika na kupendwa sana na Munyigumba. Pamoja na ushauri aliopewa na wazee kuhusu kujihadhari na mapendo na madaraka
makubwa aliyokuwa akimpa mtu huyu, Munyigumba aliongeza tena kwa kumwozesha mtu
huyu binti yake. Mtu huyu aliitwa Mwanakimamule, ila jina lake lililokuja kuwa
maarufu lilikuwa Mwamubambe au Mwambambe.
Mwambambe alikuwa jitu la miraba minne lenye nguvu sana,
inadaiwa vitani alikuwa akitangulia mbele na yeye alikuwa anawakamata adui kwa
mikono yake na kuwavunja kisha kuwatupa nyuma yake wamalizwe na askari
waliokuwa wakimfuata. Inasemekana katika
kuwa mtumwa wa kubeba madawa ya Munyigumba na yeye alitumia madawa hayo ya
mizimu hivyo ikawa si rahisi kumuua.
Katika ile vita ambapo Wangoni walimzingira Muyugumba na jeshi lake
katika mapango ya Nyamulenge, Mwamubambe na Mkwawa walikuwa bega kwa bega
walipoenda kumuokoa Munyigumba. Kiasi cha mwaka mmoja baada ya kuokolewa kutoka
kwa Wangoni, Mutwa Muyigumba akafariki.
Na bada ya muda kukatakiwa kuchaguliwe mtu wa kumrithi. Wazee wa ukoo wa Muyinga wakaingia katika wakati mgumu wa kuchagua mtu sahihi kwani
walijua wazi kuwa Mwamubambe angewasumbua, hivyo wakawa wanatafakari nani
angeweza kutawala na kuweza kumdhibiti Mwamubambe ambae alikuwa na nguvu nyingi
pamoja ya kuwa hakuwa mwenyeji. Hatimae wakamteua Muhalwike arithi kiti cha
Munyigumba, haikuchukua muda Mwamubambe alimuua Muhalwike, na wengine
husema alishawishiwa na mkewe mtoto wa Munyigumba. Mwamubambe akamtawaza ndugu
yake mmoja aliyeitwa Muhenga kutawala himaya ya Muyigumba, huyu Muhenga alikuwa
mtawala jina tu kwani Mwamubambe ndie aliyetawala haswa. Watoto wengine kadhaa
wa Muyigumba waliendelea kuuwawa na Mwamubambe, kwa usalama wake Mkwava akalazimika kuimbia himaya
iliyokuwa ya baba yake.
Kitu cha ajabu akalazimika kukimbilia Nondwa Ugogoni kwa mjomba Muyovela. Ikumbukwe
kuwa Muyovela alikimbilia Nondwa kwa kufukuzwa na Muyigumba baba yake Mkwava. Ila ni wazi Mkwava alijua kuwa Myovela hakuwa mtu wa visasi, kwani hata mdogo wake Mwengamagoha aliwahi
kumsaliti na kujiunga na Muyigumba lakini mambo yalipomuharibikia alikimbilia kwa kaka yake Myovela na akapokelewa bila kinyongo.
Ilikuwa katika wakati wa msafara huu wa kukimbilia Ugogo ambapo inadaiwa mama yake Mukwava, Sengimba, alijitupa kwenye mto sehemu iliyoitwa Kikongoma. Katika sehemu hii mto
unapita chini ya ardhi, wenyeji hupaita hapo Daraja la Mungu.
Kuna hadithi
mbalimbali kuhusu tukio hilo. Kuna wanaosema mama huyo alikuwa kwenye msafara
wa Mwanawe wakielekea Ugogoni ndipo alipoamua kujitosa kwani hakutaka kuendelea na safari na hakutaka kutekwa na Mwamubambe. Kuna hadithi nyingine za wazee wanasema mama huyo
alitekwa na Mwamubambe akawa anadaiwa akaonyeshe zilipo dawa
zilizokuwa zikimfanya mumewe Muyingumba kuweza kutawala, hivyo aliwaelekeza kuwa zipo hapo
Kikongoma, lakini walipofika aliwaambia kuwa dawa hizo hazitakiwi kuonekana na wanaume hivyo apewe
wanawake wa kumsindikiza kuzifuata, na ndipo alipofika kwenye daraja hilo
akajitosa mtoni na kujiua.
Msafara wa Mkwava ulipofika jirani na Nondwa, ujumbe ulitumwa kwenda kuomba hifadhi, Muyovela hakuwa
na kipingamizi lakini mtoto wake, Mubogamasoli, hakutaka kabisa kusikia habari
za Mkwava, kwanza alikumbusha jinsi baba yake Mkwava alivyowanyang’anya nchi,
pili Mubogamasoli alikuwa na uchungu wa kunyang’anywa mpenzi wake na Mkwava.
Kabla ya kukimbilia Nondwa, Mubogamasoli alikuwa kamchumbia Semsilamugunda,
lakini alipoondoka huku nyuma Mkwava akamuoa Semsilamugunda, ambaye ndiye alikuja
kuwa mama wa mwanae wa kwanza Sapi, baba
ya Mutwa Adam Sapi.
Ili kumtuliza mwanawe, Muyovela akamuahidi kuwa Mkwava hataletwa
Nondwa, akatuma watu wakamchukua Mukwava na kumpeleka Nzuguni, Muboga masoli akatulia.
Nae Mkwava alipofika Nzuguni akaanza kupanga namna ya
kurudi kwao kwenda kuchukua himaya ya baba yake