Pages

Monday, August 29, 2022

MKWAVA APOKELEWA NA MUYOVELA UGOGONI

 


Mukwava inasemekana alizaliwa Luhota kwenye mwaka 1855. Alipokuwa mdogo aliitwa Ntasalatsi, yaani mtu mwenye kupapasa kwa mikono na vidole anapotafuta kitu. Mkwava aliishi kwenye nyumba iliyokuwa haikosi simulizi za ushujaa wa baba yake na askari wake. Akiwa bado mdogo baba yake, Mutwa Munyigumba, alikwenda kuwa kuwapiga Wasangu na kupanua utawala wake mpaka Ng’uluhe.
Mutwa Mihwela alipokufa, mtawala ambaye alikuwa mjomba wa Muyingumba na aliwahi kumlea kwa muda mrefu,   Muyigumba alifanya kila hila mpaka binamu yake Myovela akalazimika kukimbia himaya yake na kwenda kujificha Ugogoni, na Munyigumba aliweza kuiteka kirahisi himaya hiyo na ikawa chini yake, na baadae akaweza kumnyan'ganya himaya binamu yake mwingine Mwengamagoha, mdogo wake Myovela, ambaye naye alilazimika kukimbilia alikokuwa kaka yake. Munyigumba akaweza kuunganisha koo ndogondogo nyingi kuwa chini yake na hakika alikuwa ni muhimili mwingine katika ujenzi wa kabila la Wahehe.

Munyigumba akaweka  Ivaha(ikulu) yake Muhana  sehemu iliyoka jirani na Luhota, na huko ndiko kulikuwa na kambi ya kuwazoesha vijana wa jeshi lake mbinu za vita. Kwa vile utawala wake ulipanuka sana, Munyigumba akaweka watu wake waaminifu kuwa viongozi kwenye sehemu mbalimbali alizokuwa akizitawala. Viongozi hawa waliitwa Vanzagila. Hawa pia walikuwa viongozi wa jeshi lililokuwa chini yao ambalo Mutwa angeweza kuwaita wakati wowote.

Kati ya mateka wa vita za Muyigumba alikuweko mateka mmoja wa Kinyamwezi, mateka huyu alikuwa mtoto. Mateka huyu alianza kutumiwa kwa kutumwa kubeba dawa za zilizoaminika kuwa ndizo zilikuwa za kulinda ukubwa, akaanza kuaminika na kupendwa sana na Munyigumba. Pamoja na ushauri aliopewa na wazee kuhusu kujihadhari na mapendo na madaraka makubwa aliyokuwa akimpa mtu huyu, Munyigumba aliongeza tena kwa kumwozesha mtu huyu binti yake. Mtu huyu aliitwa Mwanakimamule, ila jina lake lililokuja kuwa maarufu lilikuwa Mwamubambe au Mwambambe.

Mwambambe alikuwa jitu la miraba minne lenye nguvu sana, inadaiwa vitani alikuwa akitangulia mbele na yeye alikuwa anawakamata adui kwa mikono yake na kuwavunja kisha kuwatupa nyuma yake wamalizwe na askari waliokuwa wakimfuata.  Inasemekana katika kuwa mtumwa wa kubeba madawa ya Munyigumba na yeye alitumia madawa hayo ya mizimu hivyo ikawa si rahisi kumuua.  Katika ile vita ambapo Wangoni walimzingira Muyugumba na jeshi lake katika mapango ya Nyamulenge, Mwamubambe na Mkwawa walikuwa bega kwa bega walipoenda kumuokoa Munyigumba. Kiasi cha mwaka mmoja baada ya kuokolewa kutoka kwa Wangoni, Mutwa Muyigumba akafariki.
Na bada ya muda kukatakiwa kuchaguliwe mtu wa kumrithi.  Wazee wa ukoo wa  Muyinga wakaingia katika wakati mgumu wa kuchagua mtu sahihi kwani walijua wazi kuwa Mwamubambe angewasumbua, hivyo wakawa wanatafakari nani angeweza kutawala na kuweza kumdhibiti Mwamubambe ambae alikuwa na nguvu nyingi pamoja ya kuwa hakuwa mwenyeji. Hatimae wakamteua Muhalwike arithi kiti cha Munyigumba,  haikuchukua muda  Mwamubambe alimuua Muhalwike, na wengine husema alishawishiwa na mkewe mtoto wa Munyigumba. Mwamubambe akamtawaza ndugu yake mmoja aliyeitwa Muhenga kutawala himaya ya Muyigumba, huyu Muhenga alikuwa mtawala jina tu kwani Mwamubambe ndie aliyetawala haswa. Watoto wengine kadhaa wa Muyigumba waliendelea kuuwawa na Mwamubambe, kwa usalama wake Mkwava akalazimika kuimbia himaya iliyokuwa ya baba yake.
Kitu cha ajabu akalazimika kukimbilia  Nondwa Ugogoni kwa mjomba Muyovela. Ikumbukwe kuwa Muyovela alikimbilia Nondwa kwa kufukuzwa na Muyigumba baba yake Mkwava. Ila ni wazi Mkwava alijua kuwa Myovela hakuwa mtu wa visasi, kwani hata mdogo wake Mwengamagoha aliwahi kumsaliti na kujiunga na Muyigumba lakini mambo yalipomuharibikia alikimbilia kwa kaka yake Myovela na akapokelewa bila kinyongo.
Ilikuwa katika wakati wa msafara huu wa kukimbilia Ugogo ambapo inadaiwa mama yake Mukwava, Sengimba, alijitupa kwenye mto sehemu iliyoitwa Kikongoma. Katika sehemu hii mto unapita chini ya ardhi, wenyeji hupaita hapo Daraja la Mungu.
Kuna hadithi mbalimbali kuhusu tukio hilo. Kuna wanaosema mama huyo alikuwa kwenye msafara wa Mwanawe wakielekea Ugogoni ndipo alipoamua kujitosa  kwani hakutaka kuendelea na safari na hakutaka kutekwa na Mwamubambe. Kuna hadithi nyingine za wazee wanasema mama huyo alitekwa na Mwamubambe akawa anadaiwa akaonyeshe zilipo dawa zilizokuwa zikimfanya mumewe Muyingumba kuweza kutawala, hivyo aliwaelekeza kuwa zipo hapo Kikongoma, lakini walipofika aliwaambia kuwa dawa hizo hazitakiwi kuonekana na wanaume hivyo apewe wanawake wa kumsindikiza kuzifuata, na ndipo alipofika kwenye daraja hilo akajitosa mtoni na kujiua.

Msafara wa Mkwava ulipofika jirani na Nondwa, ujumbe ulitumwa kwenda kuomba hifadhi, Muyovela hakuwa na kipingamizi lakini mtoto wake,  Mubogamasoli, hakutaka kabisa kusikia habari za Mkwava, kwanza alikumbusha jinsi baba yake Mkwava alivyowanyang’anya nchi, pili Mubogamasoli alikuwa na uchungu wa kunyang’anywa mpenzi wake na Mkwava. Kabla ya kukimbilia Nondwa, Mubogamasoli alikuwa kamchumbia Semsilamugunda, lakini alipoondoka huku nyuma Mkwava akamuoa Semsilamugunda, ambaye ndiye alikuja kuwa mama  wa mwanae wa kwanza Sapi, baba ya Mutwa Adam Sapi.

Ili kumtuliza mwanawe, Muyovela akamuahidi kuwa Mkwava hataletwa Nondwa, akatuma watu wakamchukua Mukwava na kumpeleka Nzuguni, Muboga masoli akatulia.
Nae  Mkwava alipofika Nzuguni akaanza kupanga namna ya kurudi kwao kwenda kuchukua himaya ya baba yake

   

 

Sunday, August 21, 2022

MKWAVA ALIPOIKIMBIA NCHI YA BABA YAKE

 


Baada ya Shaka ka Senzangakhona, au kwa jina maarufu Shaka Zulu,kurithi utawala wa Wazulu baada ya kifo cha baba yake, kati ya  mwaka 1818 na 1828 alianzisha utawala wa kikatili wa kuua na kuteka tawala zilizokuwa jirani yake. Kipindi hiki kigumu kwa Wazulu kilipewa jina Mfecane, viongozi wa makabila makubwa kama Zwangendaba, Mzilikazi, na  Shoshangane wakaanza kuhamisha watu wao na kuelekea kaskazini mwa nchi yao ya awali ili kukimbia vita hizo za Shaka Zulu, nao katika kusafiri kwao wakapiga na kuteka mali za makabila walioyakuta njiani mwao bila huruma. 
Wavamizi hawa wengine wakaingia eneo sasa linaloitwa Tanzania kupitia iliko Malawi, wengine wakabaki sehemu ulipo mkoa wa Ruvuma hawa wakaja julikana kwa jina la Wangoni, jina lililokuwa kwa asili  la ujumla wa makabila mengi yaliyokuwa jirani na Wazulu.  Baada ya kutujila na kujijenga sehemu hii, mwaka 1878 jeshi la Wangoni lilipenya Ubena toka kusini mpaka kaskazini bila upinzani wowote na hatimae kuingia katika himaya ya Munyigumba.
Askari wa jeshi hili la Wangoni, walikuwa hodari wasioogopa kifo. Walitumia bangi kuondoa hofu yoyote, hivyo walifanya walichotaka katika nchi ya Ubena.
Munyigumba alikuwa hajapata nafasi ya kutayarisha majeshi yake kwa uvamizi wa watu hawa kutoka kusini,  hivyo alipojaribu kuwazuia  kazi ilikuwa ngumu sana, majeshi ya Munyigumba yalianza kusukumwa nyuma kwa urahisi kabisa. Munyigumba alirudishwa nyuma hadi karibu na Image na akalazimika kukimbilia kwenye mapango ya Nyamulenge na kujificha humo. Wangoni walipomgundua walimzingira na hakika ilionekana kuwa ndio mwisho wa Mutwa huyo.

Bahati nzuri sana  mwanae Munyigumba, Mukwava aliyekuwa na umri wa miaka 23 wakati huo alikuwa tayari askari jemadari aliyekamilika, hivyo alikusanya askari na kutengeneza jeshi imara na kuelekea Image. Alijipanga vizuri na kuwazunguka Wangoni, kisha kuwashambulia kutoka mgongoni, Wangoni hawakuwa na namna ila kujiokoa, wakakimbia wakirudi kwao kupitia Lulanga, kule wakashambuliwa tena na Mutengela aliyekuwa mutwa wa Wakinamanga, tena yeye akawafukuza mpaka ndani ya nchi yao.  Wangoni hawakuamini kipigo hicho kwani katika vita zao zote walikuwa na kawaida moja tu kushinda vita. Walirudi kwao na kutulia kwa muda mrefu.

Kiasi cha mwaka mmoja baada ya mapambano hayo na Wangoni, Mutwa Munyigumba akafariki.

Kikaanza kipindi chenye mashaka sana, kwani wakati wa uhai wake Munyigumba alikuwa na msaidizi wake ambaye alikuwa pia mkwewe. Mtu huyu aliyekuwa pande la mtu na ambaye Munyigumba alimpa mamlaka makubwa, hivyo  alikuwa akihofiwa sana. Huyu bwana alikuwa wa ukoo wa Lunyungu, kwa majina alikuwa akiitwa Mwanakimamule au Pokavilonga. Mwenyewe alijiita wa ukoo wa Mwamubambe au wengine huita Mwambambe, jina alilolitoa kutoka jina la baba yake Mubambe.
Wakina pia Muyinga walimhofu sana mtu huyu na hofu yao haikuwa bure hakuwa mtu wa kawaida. Kutokana na hofu hiyo akina Muyinga wakaacha kumtawaza Mkwava kwa vile waliona bado kijana mdogo ambaye walihisi asingeweza kushindana na hila za Mwamubambe. Hivyo wakamteua ndugu yake aliyeitwa Mhalwike awe Mutwa.  Haikuchukua muda mrefu woga wa kina Muyinga ukadhihirika,  Mwamubambe alimuua Muhalwike na kumtawaza ndugu yake aliyeitwa Mwamuhenga. Huyu alikuwa mtawala jina tu kwani mtawala rasmi alikuwa Mwamubambe.
Hapo ikalazimika Mkwawa aikimbie nchi yake mwenyewe.

Tuesday, August 16, 2022

KISA CHA MUYOVELA KUKIMBILIA UGOGONI


Mihwela alipofariki, wale watoto wake  wawili wa kiume, Muyoviligombo au Myovela na Mwengamagoha, wakaamua kugawana nchi ya baba yao na kumpa binamu yao Munyigumba mali. Munyigumba akakataa na kudai apewe eneo la kutawala. Ndugu zake wakampuuza, na yeye akajifanya kama pia hana shida kumbe alianza kupanga mipango ya chinichini ya kupata alichokuwa anakitaka. Kwanza akaanza kuonyesha ukaribu mkubwa na  Mwengamagoha, kwa kuwa huyu alikuwa na hasira za harakaharaka akawa anamtumia kumchokoza kaka yake kwa hila moja au nyingine. Alipoona hila zake hazimtii hasira Myovela akaona abadili utaratibu, siku moja akamualika Myovela amtembelee Ng’uluhe, baadhi ya Wadongwe mashuhuri waliompenda Myovela akina Luvanga, Mulala, Nyakunga, wakamkataza asiende, tena wakamshauri kuwa ni heri aondoke na watu wake na mifugo yake na kuhamia nchi nyingine, kwani ni lazima Munyigumba takuja kupiga. Myovela na watu wake wakaondoka na kutembea mpaka Izazi wakataka kuweka masikani pale, lakini wakapata habari kuwa Munyigumba na jeshi lake wanawasaka, wakalazimika kuondoka na kuvuka mto Lyambangali mpaka Ilolo, kule kulikuwa na mtawala aliyeitwa Msane, Msane aliwakaribisha Myovela na watu wake, lakini Myovela hakukaa sana hakutaka wenyeji wake aliyemkaribisha vizuri aje apewe adhabu na Munyigumba kwa ajili yake. Aliendelea na safri hadi Nyamasitu, akapumzika na watu wake pale, lakini tena akaambiwa kuwa adui bado anamfuata. Myovela aliendelea na msafara mpaka jirani na ulipo mji wa Kibakwe siku hizi, eneo hilo lilikuwa likitawaliwa na Mdemu mtoto wa Manyile, huyu aliposikia jeshi la Wadongwe lililoongozwa na Myovela linamkaribia hakungoja, aliondoka na watu wake na kukimbilia Ugogo. Wanyandewela wa Mudemu walikuwa wana haki ya kuliogopa jeshi la Myovela maana habari za ukali wa Wadongwe zilifahamika sana.  Lakini  bahati haikuwa ya Mudemu, jeshi lake  lilipofika karibu na ilipo Mvumi,  likashambuliwa na Wagogo na Wamasai na kuangamizwa karibu lote, mahala pale pakaitwa Makang’wa, na wajukuu wa waliosalimika katika maangamizi yale mpaka leo hutumia kiapo cha Kumakang’wa kukumbuka ilikolala mizimu yao.
Muyovela alitulia kwa miaka kadhaa katika makao yake mapya, watu wake wakaanza kusambaa na kuishi bila woga kwani wenyeji waliwaogopa sana hawa wageni, waliendelea kuishi na hadi leo wakazi wa maeneo ya Wota waliotokana na msafara huo wa Myovela hujitambua kuwa ni Wahehe na hufuata mila zote za Kihehe.

Myovela aliondoka tena na watu wake wengine na kuelekea  Nondwa iliyokuwa katika himaya ya Ugogo, kwenye tambarare  kusini mwa bwawa la Kinyambwa, aliafikiana na wenyeji kule na akaishi kwa raha ukiachia mapigano ya hapa na pale na Wamasai aidha kwa kuwaibia ng’ombe au walipokuwa wakiibiwa ng’ombe.

Huku nyuma Mnyigumba na Mwengamagoha wakaamua kugawana nchi. Munyigumba akamshauri Mwengamagoha akajenge ikulu yake Nzihi, wakati yeye akaendaa kujenga ikulu yake Lungemba. Myovela alipopata habari ya kinachoendelea akatuma ujumbe kwa nduguye na kumsihi  akajenge ikulu yake Luhota kwani ndiko ilikokuwa chanzo cha himaya ya baba yake, angekuwa kati ya watu wake,  Nzihi ilikuwa ni kama ugenini. Mwengamagoha  akampuuza kaka yake. Na kuanza kujenga ikulu yake Nzihi. Munyigumba akatuma kikosi cha siri kikaenda kushambulia Nzihi, mke na watoto wote wa Mwengamagoha waliuwawa, na yeye alinusurika tu  kwa kujificha kwenye shimo lililokuwa linachimbwa udongo wa kujengea ikulu yake.

Mwengamagoha alipopata nafasi akatoroka na kuelekea alikokuwa kaka yake Ugogoni. Alipofika kaka yake alimpokea vizuri lakini alimkaripia sana kwa upumbavu wake wa kutokutambua kuwa Munyigumba alikuwa adui yao wote. Mwengamagoha aliyapokea makaripio ya kaka yake vizuri lakini wake na watoto wa Muyovela waliendelea kumtania na hata kumtungia nyimbo za kejeli, hakuweza kuvumilia akahama na kuelekea Usangu na baadae Ukosikamba  hatimae akafia Udonya akiwa hana nchi,

 

 

 

 

 

 

Friday, August 12, 2022

UNAJUA JINSI MUNYIGUMBA ALIVYOPATA JINA LAKE?

 


Mtoto wa kwanza wa Kilonge na Sekindole aliitwa Mugavanalupembe. Huyu ndie aliyerithi utawala wa Ng’uluhe, lakini hakutawala muda mrefu kwani aliuwawa na Muhingile Mwangwenga kwenye ugomvi wakati wa kunywa pombe. Muhingile alitoroka na kujificha kwa muda mrefu lakini alipojitokeza kitu cha ajabu, hakuna aliyemkamata au kumhukumu.
Mtoto wa pili wa Kilonge na Sekindole aliitwa Binini. Jina hili halikupendwa sana na  kwani lilikuwa likitambulisha umbo la mtoto huyu kuwa alikuwa na aina ya kibyongo. Alikuja kujulikana zaidi kwa jina la Munyigumba au Mugohang’amwa yaani Mkuki unakamulika, kwani kwa kutumia mikuki alipata mali kama mtu mwenye ng’ombe anavyokamua maziwa.

Wakati kaka yake Mugavanalupembe alipokuwa akitawala Ng’uluhe, Binini alipelekwa kukulia kwa mjomba wake shujaa Mihwela. Mihwela alikuwa binamu ya Sekindole mama wa Binini hivyo alikuwa mjomba wake. Huko akajifunza mbinu za vita na utawala. Akaanza nae kuwa na hamu ya kutawala.

Mihwela alikuwa na watoto wa kiume wawili, Muyoveligombo na Mwengamagoha. Huyu Muyoveligombo alikuwa mwanamuziki  aliyependa kupiga ‘ligombo’, aina ya gitaa la asili ya Uheheni, na pia kuimba. Na ndivyo alivyopata jina la Muyoveligombo ambalo baadae likafupishwa na kuwa Muyovela. 

Huyu Mwengamagoha alikuwa mtu wa kukasirika kasirika na  mwenye jeuri. Mihwela aliwahi kumkemea mara kadhaa mwanae huyu kutokana kuwa na jeuri. Kuna wakati aliwateka watu wawili, Mwisaka mmoja na Mwachusi mmoja, akawatesa sana na hatimae akamuua yule Mwisaka, Mihwela alikasirika sana na kumwambia mwanae kuwa anafumua misingi ya kuunganisha  koo mbalimbali na hivyo kuwa na nguvu za pamoja na pia kwa kuwa watu hawa walikuwa mashujaa katika mapambano kadhaa aliyofanya Mihwela. Lakini Mihwela alifahamu pia kuwa Binini ndie aliyekuwa akichochea hayo ili apunguze nguvu za kumpinga wakati atakapoanza mbinu zake za kuchukua utawala.
Mihwela alimwambia mwanae Myovela kuwa apigane na Mwengamagoha na Binini wakati akiwa bado na uwezo kwani alikuwa ameota ndoto kuwa  Muyovela alikimbilia nchi ya mbali, kavu na yenye joto nje ya Uhehe. Lakini wajukuu zake watarudi Uhehe ila wakati huo watu weupe watakuwa wamefika na kuchimba ardhi na kujenga vichuguu vikubwa vyeupe. Myovela alikuwa mtu wa amani hakutaka kupigana na ndugu zake, hivyo akapuuza maagizo ya baba yake, lakini miaka mingi baadae ndoto ya baba yake ilitokea kama alivyoiota, kama tutakavyoona hapo baadae.

Wakati Binini yupo Luhota akaoa mke kutoka ukoo wa mwa Ngimba wa Ilole. Akina NGimba asili yao ni Hamitiki hivyo mpaka leo hutokeza wajukuu warefu wenye vidole virefu, masalia ya DNA ya Wahamitiki..
Binini alipoitwa kweda kwenye msiba wa kaka yake Mugavanalupembe alikataa na kusema kuwa angetaka kwanza aende kuwapiga Wasangu, kwani aliamini baada ya hapo angerudi na mali nyingi na utukufu hivyo kuchukua kirahisi himaya iliyokuwa ya kaka yake. Alikusanya vikosi vya Wadongwe wa Luhota na akapata vikosi vingine kutoka kwao Ng’uluhe, na askari wote walitakiwa kukutana Lungemba, Binini mwenyewe alipofika Lungemba,  ndugu zake akina Kindole wakamuongezea askari, akawa na jeshi kubwa. Aliingia Usangu na kuwashambulia ghafla Wasangu na kuteka mali nyingi na wanawake. Binini mwenyewe akamuua kiongozi wa Wasangu aliyeitwa Munyigumba na akatwaa jina lake kama kumbukumbu ya vita hiyo. Baada ya ushindi huo akaanza kurudi Ng’uluhe akapitia Mufindi iliyokuwa chini ya binamu yake Musambila Mwamdemu mtoto wa Chawala. Huyu alitawala Ifwagi, Mufindi na hata sehemu za Malangali. Munyigumba alipokelewa kwa shangwe na ngoma, lakini katikati ya sherehe akamchoma mkuki mwenyeji wake na kumuua na kujitangaza mtawala.  Na nia yake ya kupitia Mufindi ikadhihirika kwani alikuwa kapita ili kulipa kisasi kwani Musambila hakumpa askari wakati anaenda kupigana na Wasangu, na pia kuanza kutimiza ndoto yake ya kutawala eneo kubwa.

 

Thursday, August 11, 2022

MIHWELA MUHEHE ANASTAHILI KUITWA SHUJAA WA TAIFA

Mihwela azuia utumwa

Katika mfululizo wa historia hii nimeongelea mambo makubwa aliyofanya Mihwela mjukuu wa Chota. Lakini  mtu huyu bahati mbaya jina lake huwa halitajwi sana katika watu muhimu Uheheni, licha ya makubwa aliyowafanyia watu wa Uheheni. Tuliona jinsi alivyokuwa wa kwanza kuanza kuanzisha mpangilio wa mafunzo ya kijeshi kwa askari na alivyoweza kushinda vita kadhaa kiasi cha koo na kabila ndogondogo mbalimbali kuanza kumuita awatawale ili wapate ulinzi wa askari wake. Leo tutazungumzia jambo moja kubwa sana alilolifanywa Mihwela.

Kati ya mwaka 1820 na 1830, Waarabu walianza kuingia bara kutoka pwani na kuanza kuteka watu ili wakauzwe na kuwa watumwa kwenye mashamba ya Karafuu huko Unguja.
Kikosi kimoja cha waarabu kikaingia sehemu za Pawaga na kuteka watu wengi na kuwaweka katika makambi tayari kwa safari ya kwenda pwani kuuzwa Pwani, baadhi ya watu walioweza kutoroka walikimbia na kwenda kumtaarifu Mihwela ambaye alikusanya jeshi lake na kuweza kusafiri na hatimae kufika usiku karibu na kambi hiyo ya Waarabu. Jeshi la Mihwela lilijipanga na kuizunguka kambi ile, mapema alfajiri jeshi lile lilifanya mashambulizi na kuteketeza Waarabu wote, wakamuachia mmoja tu aliambiwa akatoe taarifa kuwa Wadongwe wamepiga marufuku biashara ya utumwa eneo lile.
Na tangu wakati ule biashara ya utumwa uheheni ilikufa, Wahehe wachache walioingia utumwani ni wale waliorubuniwa kuondoka mipaka ya Uheheni na huko kujikuta wakitekwa na kuuzwa. Wanyamwezi wanasemekana  walikuwa maarufu kwa ujanja huu wa kuwa rubuni Wahehe kuondoka katika usalama wa nchi yao.
 Waarabu walikuja baadae kufanya biashara Uheheni lakini si biashara ya utumwa, Ila ieleweke kuwa Wahehe wenyewe walikuwa na watumwa waliofanya kazi mashambani, majumbani na kwenye shughuli za uchungaji.
Kiukweli kwa hili Mihwela alistahili kuwa shujaa si wa Uheheh tu bali wa nchi yetu ya Tanzania.
Kama mnakumbuka babu yake Mihwela, Chota,  alimuua Mnyaluhwao siku ya kwanza ya kukutana nae hivyo kuzuia kuja kupingwa baadae, na Mihwela alitumia akili hiyohiyo kuzuia upinzani pale alipohisi unaweza kuja kutokea, himaya yake ikaanza kukua.
Kama tulivyoona awali alimaliza uasi wa Wasawila kwa kuwapiga wasaidizi wao Wasangu, akawaweka chini ya utawala wake Vanyandevelwa waliokuwa chini ya mtawala wao Mdemu mtoto wa Manyile ambaye baada ya mapigano kadhaa alikimbilia Wota.

Wahehe 

Jeshi la Mihwela lilikuwa na vikosi

Jeshi la Mihwela lilikuwa na vikosi vyenye watu 200 kila kikosi. Taratibu hii ya kuwa na askari 200 kila kikosi inaonekana ilikuwa ya kawaida katika Afrika, kwani miaka mingi kabla ya hapo Vanyangologo walipoingia Uheheni walikuwa wakitembea kwa vikosi vya watu mia mbili mia mbili, hata Shaka wa Wazulu jeshi lake pia lilikuwa na mfumo huo, na hata Mkwawa baadae alikuwa na jeshi lenye vikosi vya idadi hiyohiyo.

Wadongwe walipenda sana mtindo wa kuwazunguka adui usiku na kisha kuwashambulia alfajiri mapema, kila askari wa Wadongwe alikuwa na ngao iliyotengenezwa kwa ngozi ya ng’ombe iliyokuwa na urefu wa kwenda juu kimo cha askari na upana wake kiasi cha upana wa binadamu. Pia kila askari alikuwa na mikuki miwili, mmoja mwembamba alioutupa na mwingine wenye bapa nene, ulioitwa lisala, ulitumika kuchoma adui na kuchomoa kama kisu.
Mdongwe alikuwa akipigana na adui mwenye mkuki alisimamisha ngao yake, na kama ni adui waliotumia visu na mapanga kama Wahuma ngao aliishika kwa kuilaza upande kusudi kisu kisichane ngao ile kutoka juu mpaka chini. Kuna hadithi kuwa Wahehe walianza kutumia ngao baada ya kupigana na Wangoni, hii si kweli Wategeta walianza kutumia ngao baada ya mapigano yao na Wahumma na kuona Wahumma walivyofaidika na kinga hiyo

Tuesday, August 9, 2022

KABLA YA KUWA KABILA MOJA, UHEHE ILIKUWA NA VIKABILA MBALIMBALI KARIBU THELATHINI

 

Wahehe

Kabla ya Wahehe kuwa kabila moja kama linavyojulikana sasa kulikuwa na vikabila vidogovidogo karibu 30, na kila kimoja kikiwa chini ya ukoo kama ndio watawala. Tuanze na ukoo ulioitwa VaMudemu, .hawa walitawala katikati ya Ubena na Ulanga, maeneo kama  Ifwagi mpaka ilipo Malangali leo yalikuwa maeneo chini ya ya VaMudemu.  Ukoo huu unasemekana ulianzishwa na muwindaji  aliyeitwa Bugoma aliyetoka Ndweve iliyoko kwenye bonde la Ulanga. Mtiririko  wa watawala hao ulianza na Bugoma, akafuata Silonga, akafuata Nolelo, akafuata Mudemu, akaja Msambila, akafuata Mtamile na kumalizikia na Jumbe Hassan.
Kulikuwa na ukoo mwingione wenye jina la VaMudemu hawa ni wa Ndevelwa maeneo ya Isimani, hawa walikuwa ni ukoo tofauti na nilioutaja hapo awali.
Utawala mwingine Uheheni ulikuwa ni wa Ukalinga, huu ulikuweko kwenye milima ya Udzungwa. Kuna hadithi za mapokeo kuwa machifu hawa  wa Kalinga walitoka Unyakyusa, na ndio maana kuna Wanyakyusa wengi tu ni wa ukoo wa Mwakalinga, lakini pia kuna ile historia kuwa Wanyakyusa walitokana na ukoo wa Chusi  kama nilivyoeleza katika makala moja hapo nyuma.
Kuna akina Mwakalinga wengine wanasema chanzo cha ukoo wao ni Mufwimi Mwakalinga,  aliyefika Kisanga katika nchi ya Ukalinga na akampa mimba Sekikungile, na akakimbia na kumuacha binti huyo mja mzito. Sekikungile akamzaa Mupogole aliyekuja kutawala eneo la Ukalinga lililokuwa likikaliwa na Vadzungwa ambao hawakuwa na mtawala.
Mlolongo wa utawala huo ulikuwa hivi, kulikuwa na Mpogole aliemuoa Sekatefu, akafuata Lubida aliyemuoa Sepulamu, akaja  Mumehwa aliyeoa  Sekindole, akafuata Makanya aliyemuoa Semugele, akarithi Mugabe aliyemuoa  SeKindole, akarithi Mwanasindava aliyemuoa Semudalingwa, akafuatia Chotisamba aliyekuja kumzaa Hamisi aliyekuja kuwa sub chief wa mwisho  Ukalinga. Kuna kitu hapa cha kujihadhari, hadithi ya muwindaji kufika mahali  na kumpa mimba mtoto wa Chifu huwa inajirudia rudia katika simulizi nyingi za Uheheni, hivyo ni ya kuichukua kwa tahadhari kwa vile ni mapokeo. Lakini ukweli ni kuwa na kulikuwa na Wakalinga wengi katika eneo lililoitwa Ukalinga. Hii ilikuwa ni eneo mashariki mwa Mdabulo. Hivyo nyakati za mwanzo za utawala wa Muyugumba, Vakalinga nao walikuwa na utawala wao, na walikuwa wanaheshimika kiasi hata cha kufika Lugemba na kuoa akina Sekindole waliokuwa wa koo za kitawala.
Kulikuwa na kabila la Vategeta, hawa walikuwa na kiongozi aliyeitwa Nyembe au Nyembeke, Vategeta wanasemekana waliishi maeneo jirani na Ilula. Uzazi wao ni pamoja na wakina  Kihwaganise.

Ngoja nizitaje baadhi ya tawala ndogo ndogo na viongozi wao zilizokuweko kabla ya Uhehe kuwa moja;

 

1.       Igavilo, mtawala Kindole

 

2.       Savila mtawala Mandili

 

3.       Hafiwa mtawala Lyelu

 

4.       Nyandevelwa mtawala Mudemu

 

5.       Dongwe mtawala Mudung’u

 

6.       Nyimage mtawala Maginga

 

7.       Nyilambo mtawala Kitalika

 

8.       Nyilole mtawala Kihwaganise

 

9.       Tegeta mtawala Nyembe

 

10.   Fwagi mtawala Mudemu

 

11.   Ukalinga mtwala Kalinga

 

12.   Chalamila mtawala Chalamila

 

13.   Sagala mtawala Mukwando

 

14.   Sagala mtawala Mwigombe

 

15.   Nyaganilwa mtawala Mugovano

 

16.   Dzungwa mtawala Kahemela

 

17.   Dzungwa mtawala Njole

 

18.   Sagala mtawala Lwafu

 

19.   Sagala mtawala Mulandali

 

20.   Sagala mtawala Wutalo

 

21.   Dekwa mtawala Muhanga

 

22.   Dene mtawala Mulefi

 

23.   Nyamudenye mtawala  Mandongo

 

24.   Nyamugovelo (Sagala) mtawala Mutalula

 

25.   Nyang’uluhe mtawala Mududa

 

26.   Ilongo mtawala Mduda

 

27.   Ilongo mtawala Lukungu

 

28.   Kinamuyinga mtawala Muyinga


Monday, August 8, 2022

WASANGU WALITAFUNA MATETE KWA NJAA

 

Migagi

Leo tunaendelea na sehemu ya 11 ya simulizi ya historia ya Wahehe. Nitashukuru sana kama ukiwa mmoja wa atakae kuwa anafuatilia maandiko haya kwa kuwa mmoja wa followers na ikiwezekana kutoa maoni yako kuhusu unachojua kuhusu historia ya Wahehe ili tuboreshe historia hii.

Katika maelezo niliyoyatoa katika awali nilielezea mkasa wa Kindole na nduguye Chota kugombania kutawala Rugemba na hatimae Chota kuhamia Iwawa ambako pamoja na kukaribishwa kwa ukarimu mwingi aliishia kumchoma mkuki na kumuua mwenyeji wake ambaye alikuwa tayari kumuachia utawala. Sehemu iliyokuja kutawaliwa na Chota iliitwa Udongwe. Jina la Udongwe lilitokana na jina la babu yake Mnyaluwaho, akiyefahamika kama Mkilwa Mudongwe. Munyaluwaho ndie aliyekuwa mtawala aliyeuwawa na Chota, sasa kutokana na jina la babu yake, ni wazi asili yao ilikuwa Kilwa. Wajukuu wa Wadongwe wamekuwa wakijitapa kuwa wao ndio Wahehe wa asili, lakini hili lina utata kwani wengi wao walikuwa wa asili ya Wahumya (Wahamitic) ambao  hawakuwa Wabantu. Kuna wadongwe wengine asili yao Vakilwa yaani waliotoka Kilwa, wengine asili yao Vanyalyagi, wengine Vanyamahuvi, kuna Vanyandembwe ( hawa walikuwa wakidai kuwa asili ya ukoo wao ni Tembo- Ndembwe).
Lakini ni ukweli kuwa Wadongwe walistahili kuitwa kiini cha kuanzishwa kwa kabila la Wahehe. Mtu wa awali kabisa katika kujenga misingi ya Uheheni aliitwa Mihwela alikuwa mjukuu wa Chota. Miwhela alikuwa akijulikana kwa majina tofauti matatu. Aliitwa Mihwela kwakuwa alipokuwa mtoto mchanga nchi ya Udongwe ilibarikia kuwa na mvua nyingi za usiku kucha, jina lake la pili lilikuwa la Lwangwi lwa ndembwe,hii ilikuwa kwa sababu ya sauti yake kubwa iliyofika mbali alipocheka au kuongea,hivyo tafsiri ya jina lake ni kicheko cha tembo, na mwisho alijulikana kwa jina la Gingilifwili, alikuwa anafuga nywele zake nyingi na kuzifunga kisogoni!!!.
Mihwela ndie alikuwa kiongozi wa kwanza kuanza kuwakusanya askari na kuwafundisha maarifa na ujanja wa vita, jambo lililofanya Udongwe isihinde vita nyingi.
Hebu tuangalie mambo mengine makubwa aliyoyafanya Miwhela.  Wahafiwa na  Vanyamahuvi walikuwa wakiishi katika sehemu ya makutano ya mito Lyambangali na Luvaha, hawakuwa na amani kwa kuwa jirani zao Wahuma walikuwa mara kwa mara wanawashambulia. Watu hawa wakamuomba Mihwela aje kuwasaidia kumukomesha adui yao huyu.  Jeshi la Mihwela lilikuja na kuwashambulia Wahuma na kuwafukuza mpaka ng’ambo ya mto Kizigo, na pia wakanyang’anywa mifugo yao yote, tangu wakati ule Wahumma hawakuvuka tena Kizigo na Lyambangali kusumbua Uheheni. Koo mbalimbali zilikubali kumkaribisha Mihwela awatawale kwani hilo lilihakikisha amani na usalama wao toka kwa maadui.
Kuna wakati Wasangu waliingia na kuanza kuenea sehemu za Uhehe, waliingia kupitia Ilongo na kukaribishwa na Wasawila ambao walikuwa na ndoto za kumpinga Miwhela. Mihwela alishuku kuwa Wasangu wataingiliwa Uhafiwa ili kufika Udongwe kumshambulia. Kwanza akakusanya mifugo yote, ilia dui watakapofika wakose chakula, na kweli kama alivyotabiri Wasangu walipoingia uheheni wakaweka kambi mahala palipoitwa Ipagala, katikati ya Tosamaganga na Kalenga, mahala hapo palikuwa na majani ya  matete mengi, njaa zilipowazidia Wasangu walianza kuyatafuna matete kama miwa. Mihwela aliizunguka kambi ya Wasangu na kuwavamia, Wasangu wengi walikufa pale, waliotekwa wakafanywa watumwa na wachache sana waliweza kutoroka na kukimbia. Tangu ushindi ule bwawa la Kipagala likapewa jina la Idete kukumbusha jinsi Wasangu walivyofyonza matete kwa njaa.

Sunday, August 7, 2022

MAELEZO YA ZIADA KUTOKA KWA MZEE MKOCHA KUHUSU MUFWIMI

 



Simulizi kuhusu Mufwimi ni simulizi nzuri na ina uhalisia fulani. Kwa mujibu wa akina Mwamuyinga wa Image, Avanyidaha wote walikuwa wawindaji; tofauti kubwa aliyoleta Mfwimi ilikuwa ushujaa wake wa kuua mnyama mkubwa, nyati, kwa mara ya kwanza na umaarufu wa Mfwimi wa pili, alikuja na chumvi, ambayo haikuwepo. Chumvi iliwawezesha jamii ile kula nyama nyingi. Na hasa ndiyo ilikuwa kivutio cha Mfwimi kwa Mwamduda na kwa muda mfupi watu hawa wakanawiri wakawa na nguvu. Hata huyu kijana aliyezaliwa na Se Mduda licha ya uwindaji, alikuwa mtundu na jeuri kupindukia.
Wakati wa utoto wangu mwanzoni mwa miaka ya 1950, kule kwetu Image kulikuwa na utaratibu wa kupimana nguvu kwa kupigana. Kila Kijiji kulikuwa na kijogoo wa ngumi, na kulikuwa na utaratibu wa kijogoo mmoja kutawala sehemu kubwa.
Wanaume walikuwa wanapigana bila kuwa wamegombana ila tu kuonyeshana ubabe. Mwamba mmoja alikuwa anasimama mbele ya watu kwenye mkusanyika hata kama ni kilabuni au hata kusanyiko la msibani, na kujitangaza kuwa anaeona kuwa ni kijogoo ajitokeze atetee heshima yake. Na kweli ilikuwa inatokea vurugu hapo mpaka kijogoo mmoja anapatikana.
Mimi nimeanza kwenda shule 1957, kijogoo wa Image wakati huo alikuwa Mwamadate. Akikasirika mishipa ya damu ya mikononi inatokeza mithili ya mkono wa mtoto mchanga. Ngumi yake ni kifo ikimpata mpinzani kichwani. Mwamba wa kujengea nyumba ya liking'a ya vyumba 3,  anatoka nao milimani amebeba kama unyasi wakati wenzie hata kuusimamisha huo mwamba, wanasaidiana watu kadhaa!
Kwa hiyo hata majeshi ya watu hawa walioshiba nyama, maziwa na ugali wa ulezi yalikuwa na afya kweli kweli. W
aandishi wengi wa historia ya Waafrika wanasahau kuelezea jinsi lishe bora ilivyowafanya watu wa zamani wawe wakakamavu walioweza kufanya mambo mengi ya ajabu.

Saturday, August 6, 2022

MUFWIMI ALILAZIMIKA KUKIMBIA UHEHENI KUTOROKA KESI

 


Wawindaji walithaminiwa sana Uheheni kwani walikuwa chanzo cha mlo safi kwa jamii, hivyo sifa za Mufwimi zilitangulia kabla hajaingia Ng’uluhe. Alipofika Nguluhe akapokelewa vizuri na Mduda aliyekuwa mtawala wa eneo lile na kuwa mgeni rasmi wa Mutwa. Kila baada ya siku chache alikuwa akienda kuwinda na kurudi na nyama nyingi, Wahehe huita nyama hizi za porini  'mbelembo'. Kuna wakati alikuwa akipotea kwa siku kadhaa lakini hatimae akarudi tena, wenyeji wakampa jina la utani wakampa jina la Kayinguye.
Siku alizokuwa ametulia aliwafurahisha wenyeji kwa kupiga chombo chake cha muziki unachoweza kulinganisha na gitaa kilichokuwa kinaitwa Kimandinda, kilikuwa ni chombo cha muziki maarufu katika nchi ya Usagala wakati huo, nacho kama lilivyo gitaa kilikuwa na nyuzi sita.
Binti mkubwa wa Mduda alianza kumpenda Mufwimi, walianza kushinda pamoja jioni mpaka usiku mzito wakati watu wengine wamekwenda kulala, Mufwimi akimhadithia binti  yule habari zake  mbalimbali za kusisimua za maisha yake ya uwindaji. Haikuchukua muda mrefu ukaribu huo ukaanzisha mapenzi, siku moja Semduda, yaani binti ya Mduda akamwambia Muyinga kuwa anajihisi ana mimba. Mufwimi alijua kabisa kuwa kutakuwa na janga kubwa litakalomkumba pale  Mtemi Mduda atakapopata taarifa za mimba ya binti yake,  hivyo Mufwimi  akamwambia mpenzi wake kuwa kama atazaa mtoto wa kiume amfundishe kuwa mwiko wa ukoo wa Mombe ni Funo. Kisha akatoroka kuelekea kwao Ikombagulu.
Hakuna habari tena zinazosimuliwa kuhusu Mufwimi baada ya hapo, japo kuna habari zingine husema akina Mduda walimtafuta na kumuua Mufwimi kwa kosa la kumpa mimba dada yao bila ndoa,pengine hii ni hadithi tu kwani haijulikani kulikuwa na taratibu gani za kuishi  mtu na mzazi mwenzie zama hizo,
Mduda alimpa mjukuu wake jina la Mwamuyinga, yaani mtoto wa yule anayetangatanga. Mwamuyinga nae alikuwa na kuja kuwa muwindaji hodari kama baba yake, na pia alikuwa na busara sana, inaonekana alikuja kuwa kipenzi cha babu yake, hivyo alikuja kurithi sehemu ya utawala wa Babu yake, baada ya kifo cha Mduda.

Kuna hadithi za mapokeo kuhusu watawala waliokuja kumrithi Muyinga huyu wa kwanza, lakini nyingine ni wazi ni za kubuni, na pengine nyingine zimebadilika kutoka na kuwa zimekuwa zikirithiwa kwa kuhadithiana. Kilicho wazi ni kuwa kwa vyovyote Muyinga hakuweko kabla ya mwaka 1760, hivyo kutaja majina mengi ya warithi wa Muyinga wa kwanza na kudai kuwa wengine walitawala mpaka uzee sana  kunakosa mashiko kutokana ma  muda. 
Huwa majina kama Kitova, Lalika,  Mdegela, Kilonge hutajwa katika orodha ya watawala warithi wa Muyinga, lakini kuna wenye kudhani kuwa Kitowa ni jina jingine tu la Muyinga wa kwanza, na Lalika ni jina la mdogo wake Mdegela aliyekuwa babu mzazi wa Mkwava. Kuna wanaosema Kitoa na Mdegela ni jina lamtu huyohuyo mmoja, wengine husema Mdegela alikuwa mtoto wa Kilonge, na wengine husema Kilonge alikuwa mtoto wa Mdegela, na huo ndio mchanganyiko wenyewe. Kwa kuendeleza historia tukubali kuwa Kilonge alikuwa mtoto wa Mdegela.
Inasemekana kuwa akina Muyinga walikuwa wakioa katika ukoo wa  Mveyange, Kindole na Vanyamahuvi. Mpango huu ulikuwa tofali moja katika ujenzi wa kabila moja la Wahehe..
Kilonge alimuoa binti mmoja wa Kindole, ukumbuke kuwa Kindole alikuwa mtawala wa Lungemba baada ya msuguano na kaka yake Chota, hivyo baada ya Kilonge kumuoa Sekindole, binti huyo alipewa na baba yake askari 200 wa kumsindikiza na kumlinda na hatimae wawe walinzi wa sehemu aliyotawala Kilonge. Labda niongeze neno hapa, Wahehe walikuwa na utaratibu wa kuwa na vikosi vya askari mia mbili mia mbili. Baada ya kukabidhiwa  jeshi hili na mkwewe,  Kilonge akaanza kutamani  kutawala Nguluhe yote kama ilivyokuwa enzi za Mduda, hivyo akamtimua kaka yake aliyeitwa  Manga, ambae akalazimika  kukimbia na wafuasi wake ambamo pia walikuweko Watemikwila.
Kundi hili lilikimbia mpaka nyanda za juu za Ubena, sehemu ambayo sasa inaitwa Masagati. Jina hili lilitokana Mwarabu mmoja aliyeanzisha shamba la miti ya mpira na kuamua kupaita mahala hapo Muscat akikumbuka nchi aliyotoka, ugumu wa matamshi  ya jina hilo ukapafanya hapo paitwe MASAGATI. .   

Thursday, August 4, 2022

WAHABESHI , WAZIGUA NA WAJUKUU ZAO WAHEHE

 


Kipindi kilekile ambacho Vanyangologo walikuwa wakitoka ilipo Kenya na kuelekea kusini hadi kufika Uheheni, Mhabeshi mmoja alianza safari kwa kutumia punda, safari yake ilikuwa  kuelekea kusini mwa Uhabeshi. Alishuka chini mpaka kufika Ukambani ambapo alipata mke wa Kikamba na kuzaa nae watoto wakiwemo wanaume watatu.
Hawa watoto walipofika umri wa utu uzima, nao wakaondoka kwao nakusafiri kuelekea kusini zaidi kama alivyofanya baba yao, hatimae wakaingia  nchi ya Uzigua ambako wakaoa na kisha kuendelea na safari kuelekea kusini zaidi wakifuata njia ile ile waliopita Vanyagologo miaka kadhaa nyuma,
Hatimae waliingia Usagala na kufanya makazi yao mahala palipoitwa Ikombagulu, kule kwenye michoro ya kale ya kwenye mapango. Hapo wakaanzisha ukoo uliokuja kuitwa Mombe. Kuna wanaosema jina hili linauhusiano na Mombo iliyoko karibu na Lushoto. Kuna Wazigua wengine walikuja kuwafuata baadae nao hatimae walikuja kuwa Wahehe ambao hujulikana kwa 'mwidikiso' wa Vanyamsigula.
Katika wale watoto watatu wa yule Mhabeshi aliyeoa Mkamba, akina Mombe hukumbuka  jina la mtoto mmoja tu nalo ni Mubunsugulo. Akina Mombe husisitiza kuwa Mubunsugulo alikuwa mweupe, pengine weupe uliotokana na muingiliano wa Wareno na Wahabeshi, miaka mingi nyuma. Kwenye mwaka 1520 Wahabeshi waliomba msaada wa Wareno katika vita ya kidini iliyokuwa inaendelea, kikosi cha askari 400 wa Kireno waliweka makazi yao kwa miaka kadhaa katika nchi ya Uhabeshi.
Inasemekana Mubunsugulo alikuwa na watoto watatu. Wa kwanza Nguluchawangi,  huyu pia aliitwa Manga na alihamia Masagati, wa pili alikuja itwa Mufwimi yaani muwinaji, na wa tatu ni Ngwila ambaye alikuja kurithi kwa baba yake utawala wa  nchi kutoka Ikombagulu hadi Ifakara. Taarifa hii hupingwa na wazee wengine ambao husema Manga alikuwa kaka yake Kilonge, babu yake Mkwava na Ngwila alikuwa Mkamba aliyekuwa binamu yake Mubunsugulo. Hata hivyo kundi la wajukuu wa Ngwila lilihamia iliko Pawaga siku hizi. Vanyamsigula wengine walikwenda kuishi Wota kaskazini mwa Lyambanngali na wengine walikuja kuhamia Ugogo wakiwa na makundi makubwa ya ng’ombe.
Kuna hadithi moja ya ajabu sana kuhusu hawa waliohamia Ugogo. Kiongozi wao alipata ugonjwa wa  ndui, hivyo watu wake wakamtenga na kuhama na kumuacha peke yake. Siku moja radi kubwa ilipiga na kuwatisha  ng’ombe ambao walikimbia na kurudi makazi yao ya zamani alikoachwa yule kiongozi mwenye ndui. Yule kiongozi mwenye ndui aliweza kuanza kuishi kwa kunywa maziwa na kumuomba mizimu ya kwao hadi akapona ndui. Baada ya mkasa huu wa ajabu, Wamasai waliokuwa wakiishi jirani na maeneo hayo walimchagua awe Laibon wao.na kumpa jina la Arheringisho maana yake Ng’ombe mweusi mwenye nyota nyeupe kichwani.
Hadithi hii inaeleza kwa sababu gani Wamasai wa Ugogoni hujitapa kuwa asili ya mkuu wao ni moja na ile ya Mkwawa.
Siku moja Mufwimi mtoto wa Mubunsugulo, aliondoka Ikombagulu  kwenda kuwinda, akapitia Usagala, akapanda milima ya Udzungwa na kutokea Ng’uluhe, nchi ya udongo mwekundu. Wakati huo Nguluhe ilikuwa inatawaliwa na Mduda, huyu alikuwa Msagala aliyetokana na wale watu weupe  waliofukuzwa na Vanyangologo kama nilivyohadithia huko nyuma. Asili yake hiyo inathibitishwa na mwiko wa ukoo huo iliyokuwa  boga lililoitwa lilangala, ambalo huwa na rangi nyekundu ya kung’aa inayokumbusha asili ya ngozi yao.
Hata jina la ukoo huu huitwa pia Ginga yaani fuga nywele, ikimaananisha watoto wao walikuwa wakikumbushwa kufuga nywele zao ambazo zilikuwa  kama za kizungu au za kiarabu. Watoto wa Mduda walioa katika koo za Mveyange na Wategeta, walizaliwa watoto shupavu ambao hawakukubali kutawaliwa, wakaja kuitwa Vatemikwila, pengine kutokana na swali walilopenda kuuliza mtu yoyote aliyejifanya mtawala, Mtemi kwiya? Maana yake  We Mtemi wa wapi?

 

 


Wednesday, August 3, 2022

UNAJUA CHANZO CHA JINA MTAGE?

 


Kamwene vanyalukolo, leo naomba niendelee kutaja makundi mengine makubwa ya watu walioingia Uheheni. Kundi la kwanza ni lile lililotokea  Ukimbu, hili kundi linadhaniwa liliingia wakati mmoja na Wakilwa. Kundi hili lilikuwa likijiita Vanyandembwe, ndembwe ni tembo, na Vanyandembwe walikuwa wakidai asili yao ni tembo.
Kwa nyakati hizi ni ukoo wa akina Ugulumu na Ifweni ndio wajukuu wa kundi hili la Vanyandembwe. Baadae sana liliingia kundi jingine kutoka Ukimbu hili liliongozwa na  Mufilinge aliyekuwa mtoto wa Musawila aliyekuwa mtawala wa Ukimbu wakati huo. Na kwa sababu hiyo ukoo wa Mfilinge huitwa Vasawila, wao walikuja kuishi sehemu za kutoka  Makungu mpaka jirani ya Wasa na eneo hilo lilikuja julikana kama Usawila.
 Inawezekana walikuwa na uhusiano na Vanyamahuvi kwani , walipofika Uheheni walikaribishwa na Vanyamahuvi na kupewa eneo la  Makungu watawale, lakini baada ya muda mfupi waliongezeka na kutawala kuanzia Kiponzelo mpaka Malangali, jambo lililowaletea uadui na ukoo wa Nyilowa na Nyakunga ambao hatimae walihamia Uhafiwa na Udongwe.
Hawa Wasawila walipoingia uheheni walikuwa wakivaa aina ya nguo iliyotengenezwa kwa magamba ya miti yaliyotwangwa,  wenyeji wakawaita Vanyamwenda.
Pia walikuwa waganga wazuri hivyo wanawake zao wakapewa mwidiko ( muitikio) wa Ganga, wakati wanaume zao waliitika kwa Mikwile au Nyasite.
Wasawila waliendelea kukumbusha kuwa wao ni Wakimbu. Makundi mengine yalichukua lugha ya wenyeji na hakika Kihehe kilipata mchango wa maneno kutoka lugha nyingi za wageni walioingia.
Kwa mfano Wakimbu ndio walioleta neno Mtemi,  ambalo walilikopa ktoka kwa jirani zao Wanyamwezi. Wahehe wakaanza kutumia neno Wutemaa kumaananisha utawala, kabla ya hapo walikuwa wakitumia neno Wumutwa ambalo lilitoka kwa Wabena.
Kwa Wahehe jina Mtemi hutumika likiwa na maana mkata shauri au hakimu, kutema ni kukata. Wahehe waliamini mtunga sheria asiyehukumu na kuadhibu hawezi kuheshimiwa.
Lugha ya Kihehe imebadilika sana, kwa mfano ,nakumbuka wimbo ambao babu yangu alinifundisha na kunambia kuwa ulikuwa wimbo wa askari wa Kihehe walipotoka vitani, wacha niuimbe mwenye kuweza kuutafsiri tafadhali fanya hivyo kwenye sanduku la Comment hapo chini;
 Mitela kimalimali na manyile mtalavande
Oh Likalikasela 
Oh likoko ngomba mitela

Ukoo wa Ndondole hasa akina Kindole walisifika kupenda kujikweza kuwa wao ni ukoo wenye hadhi,  wanaume walijiita Mulugu Mutavangu, maana yake kiongozi wa wapiganaji na wanawake wakajiita Vanyatage yaani waliotupwa, hii ilikuwa kukumbusha kitendo cha Kindole kung’ang’ania kutawala Lungemba, na kumtupa kaka yake Chota aliyekwenda kutawala kwa Mnyaluhwao.
Baadae Wahehe waliendeleza utamaduni huu kwa kumuita mwanaume  mwenye hadhi Mulugu na mwanamke mwenye hadhi Mtage.

Tuesday, August 2, 2022

JE UNAJUA CHANZO CHA USEMI 'LUSUNGU LWA MNYALUHWAHO'?



Baada ya vurugu ya Vanyangologo kwisha, nchi ya Uhehe ikatulia kwa muda na ikaendelea kupata wageni kutoka sehemu nyingine mbalimbali, waliokuja kuhamia Uheheni.  Kutoka Ukimbu yalikuja makundi mawili, moja likiongozwa na Ndondole na Muntsali na la pili liliongozwa na Mwigiha na Nyilowa. Kutokana na maelezo ya wahenga, watu hawa hawakuwa weusi,  walikuwa weupe japokuwa weupe wao si ule wa wazungu.

Kundi la Ndondole na Muntsali likaja kuhamia panapoitwa Panunu karibu na lilipo kanisa Katoliki la Malangali, na kundi la Mwigiha na Nyilowa likaenda kuweka maskani yake Uhafiwa. Kuna uwezekano mkubwa kuwa makundi haya yalikuwa na chanzo kimoja kwani mwiko wa kundi la Mwigiha na Nyilowa, ulikuwa ni ule ule wa kundi la Muntsali na Ndondole , mwiko wao ulikuwa ng’anga au  Kanga. Pia hata mwidikiso wao wote ulikuwa Nyamahuvi. Baadae Nyilowa  aliongoza kundi lake na kwenda kufanya maskani yao Lutemi na kule Makungu. Kati ya watoto wote wa Nyilowa, aliyekuja kuwa maarufu zaidi ni Nyakunga.  Watoto wa Mwigiha walikuja kuwa watawala., mtoto wake wa kwanza aliitwa Lyelu, huyu  alitawala kuanzia Welu hadi Pawaga, na mtoto wake  mwingine aliitwa  Mwano, huyu  alitawala kuanzia kilima cha Utinde, kaskazini mwa Kalenga, sehemu ya ilipo Iringa sasa na mpaka  sehemu za Nduli, na  sehemu kadhaa za Pawaga mpaka Manyile juu ya Ndewela.  Kuna akina Nyakunga mpaka karibuni wamekuwa wakizaliwa na kuwa na nywele nyekundu au zenye rangi ya dhahabu. Na kuna wajukuu wa akina Mwano walio na nywele za singa laini za kahawia, za kukaribiana na rangi za nywele za wazungu.
Muntsali alikuja kuongoza wafuasi wake wakahamia Wanging’ombe, huko akawa mtawala. Mwanamke mmoja kutoka ukoo wake alikuja kuolewa Uwanji na mwanae ndie akaja kuwa Chifu Merere wa kwanza aliyetawala, huyu aliwatawala Wasangu na Wasafwa.
Jina la awali la Ndondole lilikuwa Benna, siku hizi wajukuu wanaume wa ukoo huitwa kwa mwidikiso wa Benaa na wanawake Nyatende. Ndondole pia alikuwa na watoto wengi lakini waliokuja kujitokeza zaidi katika historia ya Wahehe ni Chavala na Kimamu.
Chavala alikuja kuhamia Mufindi, na ukoo uliokuwa unatawala kule, ukoo wa Kavindikadodi, ukamuachia nchi atawale. Akapata mke Sekiduku, ambaye alipata mimba lakini wakati wakati wa kuzaa mtoto akawa hatoki, hivyo wakalazimika kufanya kile ambacho ni cha kawaida siku hizi, nacho ni kutanua njia kwa kumchana, na mtoto akazaliwa salama. Kuchana kwa Kihehe ni kudemula, hivyo mtoto huyo akaitwa Mdemu.
Watu wa ukoo wa Chavala, hasa akina Mdemu, huwa na si weusi huwa na rangi nyepesi na nywele nyekundu. Wanawake wa ukoo huu huitika kwa mwidikiso wa  Gogo. Sifa moja ya ukoo wa Chavala ni uganga wa kiasili.
Huyu mtoto mwingine wa Ndondole, yaani Kimamu, alizaa watoto wengi , lakini historia ya Uhehe  inawakumbuka sana  wawili Chota na Kindole .  Hawa walijulikana sana kwa uganga wa kuzindika nyumba, mashamba na hata nchi nzima. Kwa sababu hiyo waliitwa na watawala huku na kule kwenda kuwa zindika, hata Wakilwa waliokuwa wakitawala sehemu mbalimbali za Uheheni,  waliwaita ili wazindike nchi yao ili kusitokee tena kuingiliwa na maadui kama wale waliokuwa wakiteka watumwa au kushambuliwa tena na Vanyangologo.
Wakati mmoja  Chota na Kindole waliitwa  Lungemba ili wakatawale,  ili watu wawe na uhakika wa usalama. Chota aliyekuwa mkubwa akamwambia mdogo wake achukue ng’ombe na yeye achukue nchi. Kindole alikuja juu na kuanza kuchoma mikuki hovyo ng’ombe aliokuwa kakusanyiwa, huku akuisema ‘Sitaki ng’ombe nataka nchi’. Watu waliweza kuwatuliza na kumuomba Chota amuache mdogo wake atawale Lungemba na yeye akatawale Iwawa, nchi iliyokuwa na rutuba na wenyeji wake walikuwa tayari kumpokea awe mkuu wao. Chota akaafiki wazo lile.
Iwawa wakati huo ilikuwa ikitawaliwa na Munyaluwaho, mjukuu wa Mdongwe na Mkilwa wa ukoo wa Kavindikadodi. Mnyaluwaho aliposikia Chota anakuja akamuandalia karamu na kumpokea vizuri sana. Walipokula na kushiba na watu wakiendelea na sherehe ya kumpokea mkuu mpya, Chota, ambaye inasemekana alikuwamtu mwenye miraba minne, na alikuwa na ndevu ndefu za singa, alikuwa mweupe kiasi cha watu kumuita mwelu, alichukua mkuki na kumchoma nao Mnyaluwaho moyoni na kumuua palepale.  Wenyeji walitimka mbio hovyo,  ndugu wa Mnyaluwaho, akina Kavindikadodi wakakimbia kabisa nchi na kuhamia Udzungwa.  Hivyo Chota akaanza kutawala akiwa na uhakika hatapata upinzani kutoka kwa ndugu wa marehemu. Himaya ya Chota ilianzia Iwawa mpaka ilipo Iringa, na hata sehemu za Udongwe. Makao yake yakawa Luhota iliyokuwa katikati ya Udongwe.  Kuanzia wakati huo Wahehe walipata msemo ‘lusungu lwa Munyaluhwao’…yaani ukarimu wa Mnyaluhwao ulivyomponza….ili kuonya hatari za ukarimu kwa usiemjua vizuri….. Wahusika toeni maoni

 

 

Monday, August 1, 2022

JE UNAJUA MWITIKO AU MWIDIKISO WA MGONANZI ULITOKA WAPI? SOMA HAPA

WAZEE  wa zamani wa Kisambaa walikuwa wakihadithia kuwa kuna wakati kundi kubwa la Wahumba lilipita nchini kwao likielekea Kusini, ilikuwa ni wakati Waarabu wa Oman chini ya Mfalme wao Said Bin Sultan walipokuwa wakiwashambulia Wareno katika ngome  yao  Fort Jesus kule Mombasa. Kwa tarehe hizo ina maana Wahumba hao walipita Usambaa kati ya tarehe 13 March 1696 na 13 March1698.  Wahumba hao walikuwa wakiongozwa na Wahabeshi.  Wahumba hawa walikuwaa wametoboa masikio yao na kuyarefusha hadi kufikia karibu na mabega na hivyo masikio yalifanana na aina ya pembe za  ng’ombe ambazo hupinda na  kuangalia chini, pembe za aina hiyo hiyo huitwa Ngologo, hivyo Vahumba hawa walipoingia Uheheni walikuja julikana kama  Vanyangologo.
Vahumba hawa waliingia Uheheni kupitia Wota kisha wakavuka  Lyambangali na kuingia Ugunda. Kama nilivyokuhadithia katika masimulizi huko nyuma, Ugunda ilikaliwa na watu weupe ambao wenyeji waliwaita Valangi.
Wahumba hawa waliwashambulia Valangi na kukawa na mapigano makali watu wengi pande zote wakapoteza maisha na Valangi wakalazimika kukimbia na ndipo wakahamia Singida kama nilivyokuhadithia hapo awali.
Pale Ugunda kulitapakaa sime za Vahumba waliouwawa, na kwa kuwa wahehe huita sime Mage, mahala pale pakaitwa Image mpaka hivi leo.
Vanyangologo waliendelea na safari yao ya kusaka watu weupe huku wakiacha ndugu zao wengine kuwaangalia majeruhi pale Image. Safari hiyo ya kuwaska na kuwauwa watu weupe iliendelea mpaka Ilongo, Ubena, na hata Ukimbu.
Kitu cha ajabu ni kuwa Vahumba hawa hawakushughulika na Vakilwa, hivyo Vakilwa walikuja kuanza kutawala sehemu nyingi ambazo hawakuguswa.
Wale Vanyangologo waliobaki Image walianza mahusiano na wanawake wa Usagala, Hivyo katika sehemu za Image na Ilole kukawa na koo za wahehe ambao wanafanana na Wamasai kwa umbo, na sura zao za kuchongoka.
Wengi hukataa kuwa asili ya kizazi chao ni  Vahumba lakini wanadai asili yao ni Hamitic. Lakini Humma maana yake ni Hamitic. Akina Ngimba wa Ilole asili yao ni Vahumba. Itakumbukwa kuwa  mama mzazi wa Mutwa Mkwava alikuwa Sengimba.
Ukoo wa akina Sambala asili yao ni Wahamitic, hata mwitiko au mwidikiso wao ni Mugonanzi , maana yake mwenye kulala sehemu mbalimbali au mhamaji, kwa Kiingereza tungesema nomad na hiyo ndiyo ilikuwa sifa ya Vahuma.
Wale wasagala weupe hawakukwepa kusakwa na Wahumba, wengine wao walikimbilia Wota kwa kuvuka Lyambangali,hawa wakaja kujiita  Mlowoka. Kuna walowoka wengine walikuja kurudi Uheheni  kama ukoo wa Fivawo na Makombe wa Tanangozi na Iwawa. Mliotajwa mnasemaje?

 

 

 

 


STAT COUNTER