Pages

Monday, August 8, 2022

WASANGU WALITAFUNA MATETE KWA NJAA

 

Migagi

Leo tunaendelea na sehemu ya 11 ya simulizi ya historia ya Wahehe. Nitashukuru sana kama ukiwa mmoja wa atakae kuwa anafuatilia maandiko haya kwa kuwa mmoja wa followers na ikiwezekana kutoa maoni yako kuhusu unachojua kuhusu historia ya Wahehe ili tuboreshe historia hii.

Katika maelezo niliyoyatoa katika awali nilielezea mkasa wa Kindole na nduguye Chota kugombania kutawala Rugemba na hatimae Chota kuhamia Iwawa ambako pamoja na kukaribishwa kwa ukarimu mwingi aliishia kumchoma mkuki na kumuua mwenyeji wake ambaye alikuwa tayari kumuachia utawala. Sehemu iliyokuja kutawaliwa na Chota iliitwa Udongwe. Jina la Udongwe lilitokana na jina la babu yake Mnyaluwaho, akiyefahamika kama Mkilwa Mudongwe. Munyaluwaho ndie aliyekuwa mtawala aliyeuwawa na Chota, sasa kutokana na jina la babu yake, ni wazi asili yao ilikuwa Kilwa. Wajukuu wa Wadongwe wamekuwa wakijitapa kuwa wao ndio Wahehe wa asili, lakini hili lina utata kwani wengi wao walikuwa wa asili ya Wahumya (Wahamitic) ambao  hawakuwa Wabantu. Kuna wadongwe wengine asili yao Vakilwa yaani waliotoka Kilwa, wengine asili yao Vanyalyagi, wengine Vanyamahuvi, kuna Vanyandembwe ( hawa walikuwa wakidai kuwa asili ya ukoo wao ni Tembo- Ndembwe).
Lakini ni ukweli kuwa Wadongwe walistahili kuitwa kiini cha kuanzishwa kwa kabila la Wahehe. Mtu wa awali kabisa katika kujenga misingi ya Uheheni aliitwa Mihwela alikuwa mjukuu wa Chota. Miwhela alikuwa akijulikana kwa majina tofauti matatu. Aliitwa Mihwela kwakuwa alipokuwa mtoto mchanga nchi ya Udongwe ilibarikia kuwa na mvua nyingi za usiku kucha, jina lake la pili lilikuwa la Lwangwi lwa ndembwe,hii ilikuwa kwa sababu ya sauti yake kubwa iliyofika mbali alipocheka au kuongea,hivyo tafsiri ya jina lake ni kicheko cha tembo, na mwisho alijulikana kwa jina la Gingilifwili, alikuwa anafuga nywele zake nyingi na kuzifunga kisogoni!!!.
Mihwela ndie alikuwa kiongozi wa kwanza kuanza kuwakusanya askari na kuwafundisha maarifa na ujanja wa vita, jambo lililofanya Udongwe isihinde vita nyingi.
Hebu tuangalie mambo mengine makubwa aliyoyafanya Miwhela.  Wahafiwa na  Vanyamahuvi walikuwa wakiishi katika sehemu ya makutano ya mito Lyambangali na Luvaha, hawakuwa na amani kwa kuwa jirani zao Wahuma walikuwa mara kwa mara wanawashambulia. Watu hawa wakamuomba Mihwela aje kuwasaidia kumukomesha adui yao huyu.  Jeshi la Mihwela lilikuja na kuwashambulia Wahuma na kuwafukuza mpaka ng’ambo ya mto Kizigo, na pia wakanyang’anywa mifugo yao yote, tangu wakati ule Wahumma hawakuvuka tena Kizigo na Lyambangali kusumbua Uheheni. Koo mbalimbali zilikubali kumkaribisha Mihwela awatawale kwani hilo lilihakikisha amani na usalama wao toka kwa maadui.
Kuna wakati Wasangu waliingia na kuanza kuenea sehemu za Uhehe, waliingia kupitia Ilongo na kukaribishwa na Wasawila ambao walikuwa na ndoto za kumpinga Miwhela. Mihwela alishuku kuwa Wasangu wataingiliwa Uhafiwa ili kufika Udongwe kumshambulia. Kwanza akakusanya mifugo yote, ilia dui watakapofika wakose chakula, na kweli kama alivyotabiri Wasangu walipoingia uheheni wakaweka kambi mahala palipoitwa Ipagala, katikati ya Tosamaganga na Kalenga, mahala hapo palikuwa na majani ya  matete mengi, njaa zilipowazidia Wasangu walianza kuyatafuna matete kama miwa. Mihwela aliizunguka kambi ya Wasangu na kuwavamia, Wasangu wengi walikufa pale, waliotekwa wakafanywa watumwa na wachache sana waliweza kutoroka na kukimbia. Tangu ushindi ule bwawa la Kipagala likapewa jina la Idete kukumbusha jinsi Wasangu walivyofyonza matete kwa njaa.

1 comment:

STAT COUNTER