Pages

Sunday, April 11, 2010

Aga Khan 3

Niligusia hapo awali kuwa nilipoingia Form One nilikuta wanafunzi wengi kutoka Mwanza wakiwa Form Two, ni karibuni tu ndio nilikuja fahamu sababu. Usitishwaji wa darasa la nane ulianza kwa awamu tofauti katika Kanda mbalimbali, kuna kanda ambazo zilianza kufuta darasa la nane tangu 1965, wakati Kanda ambayo Iringa ipo walifuta darasa la saba 1967. Hivyo basi wale wanafunzi waliolazimika kuingia Form One kutoka mikoa ya kaskazini walipelekwa mikoa ya kusini kama Iringa ambako kulionekana kuna nafasi, tatizo ni kuwa nafasi hii haikupatikana kwa wanafunzi wa ziada waliomaliza darasa la saba na la nanewaliotoka kusini, hivyo wengi kukosa nafasi ya kuendelea iliyokuwa imechukuliwa 1966. Pamoja na kuonekana ni jambo la kawaida lakini matokeo ya nafsi hizo kukosekana kwa wanafunzi wa kusini yanaonekana mpaka leo.

Friday, April 9, 2010

Aga Kha Secondary 2


(Picha ya juu Hostel ya wanafunzi wa Kihindi, chini madarasa Aga khan)
Chini ya Headmaster Mr Sheikh, ambaye baadae alitoka na kwenda kuanzisha Highland Secondary School, tulianza masomo. Mi nadhani nina bahati na herufi B. Darasa la kwanza na la pili nilisoma Government Primary Std IB na IIB, nikahama shule na kuingia Consolata Primary na kusoma IIIB na IVB, nilipofika Aga Khan Secondary nikasoma Form 1B na Form 2B.
Form 1B lilikuwa darasa lenye watu wa kukumbuka maana walikuwa na mengi waliyoyafanya katika kipindi chote cha O level. Namkumbuka Andrew 'Kojo' au 'The artfull dodger', alijipa jina hili baada ya kusoma kitabu cha Oliver Twist, na kujikuta ana uwezo wa kutoroka darasani wakati mwalimu anaandika ubaoni. Walikuweko Frank na Japhet vijana wawili wa Kichaga waliokuwa mabingwa wa draft, hao waliweza kucheza draft hata katikati ya kipindi wakati mwalimu anafundisha. Eberhard, bingwa wa kusoma. Abasi alieacha shule baada ya miezi michache akisema haelewi kitu kinachoendelea . Tulikuwa na waalimu wahindi , waswahili, Mu Irish, Mrusi, Wamarikani, Mnorwegian. Kazi kubwa ilikuwa. Kati ya waalimu wa kukumbukwa alikuweko Mr Dhanani, huyu alikuwa mwangalizi wa Hostel ambayo kwa wakati huo ilikuwa ya Wahindi watupu, na pia alikuwa mwalimu wa Book keeping. Utamu wa mwalimu huyu ni Kiingereza chake cha kihindi na jinsi alivyokuwa anashindwa kabisa kutamka majina ya waswahili, rafiki yangu Mbembati aliishia kuitwa Mabemabati kila siku, Mr Dhanani alikuwa na mwandiko mzuri sana, mpaka wengi tukawa tunajitahidi kuuiga.
Katika kipindi hiki kukaanzishwa gwaride la Kimapinduzi, wataalam wa gwaride hili walikuja kutoka Zanzibar. Amri za gwaride hili zote ziliishia neno z,..Nyumaz geuka, kushotoz geuka, kuliaz geuka. Lilikuwa gwaride la mapozi na silaukakamavu kama lile la jeshi. Kuna mambo ya kuchekesha lakini kila mara ilikuwa huruma kuangalia watoto wa kihindi wakijaribu kutembea katika paredi, kila wakijaribu walijikuta mkono wa kushoto na mguu wa kushoto vinaenda pamoja na mguu wa kulia na mkono wake vinaenda pamoja.

Thursday, April 8, 2010

Aga Kha Secondary 1


Mwaka 1967 ndipo darasa la nane lilipofutwa Mkoani Iringa, hivyo waliokuwa std VIII walifanya mtihani na std VII tayari kwa pamoja kusubiri kuchaguliwa kuingia Form One. Kati ya wanafunzi wanane tuliochaguliwa kuingia sekondari, waswahili tulikuwa wawili, Mheshimiwa aliyekuwa Mbunge Kisyeri Chambiri na mimi. Wengine sita walikuwa wahindi. Na wote tukachaguliwa kuingia Aga Khan Secondary Iringa. Kuingia sekondari ni experience nyingine. Nilikutana na rafiki zangu niliyoachana nao Consolata, kama Emmanuel 'Katuluta', Chesus, Naboth, Nuhu, na hata wale waliotutangulia kama Gerald, John Mzungu, Kandoro, na wengine wengi. Siku ya kwanza nakumbuka kabisa tulipewa mafyekeo na kuanza kufyeka majani,kila mtu akijihisi kuwa katika hatua mpya ya maisha. Mwaka 1966 ulikuwa umeanzishwa mpango ambao uliweza kufuta kabisa ukabila, kwa kuchanganya watu toka mkoa mmoja kwenda mwingine hivyo form 2 tulioikuta ilikuwa na wanafunzi wengi sana kutoka Mwanza hususan Wasukuma. Mchanganyiko huu ulifanya maisha ya shule ile kuwa na kumbukumbu nyingi sana za furaha. Rafiki yangu Kisyeri ambaye alikuwa na bongo inacheka sana hasa kwenye mahesabu aliamua kuhamia shule ya Ufundi Ifunda, mwenyewe akiwa na picha kamili kuwa anataka kuwa engineer. Nakumbuka barua zake za kwanza kwangu akiniandikia wanaproject ya kutengeneza Hoovercraft. Hiki ni chombo kinachoweza kutembea hewani majini na kwenye nchi kavu. Nasi tukaanza maisha ya form one tukiwa na waalimu wa Kimarekani waliokuwepo kutokana na mpango wa Peace Corps. Kasheshe ndipo lilipoanza, kufundishwa Kiingereza na Mmarekani, anamaliza kipindi hata akiwauliza 'Did ya understand?' Hamjui anasema nini, wala alikuwa anasema nini kipindi kizima. Maliwato

Tuesday, April 6, 2010

Aga Khan 2


Siku za sikukuu za Kitaifa hazikuwa nzuri kwa watoto wa Kihindi, maana ndio siku za kukutana na wanafunzi wa shule nyingine siku hiyo watavutwa nywele watataniwa,jamaa zangu wa Kisingasinga watavuliwa vilemba, basi ikikaribia siku ya sikukuu kama vile Muungano au Sabasaba, utaona waswahili tunaanza kukaribishwa kile chakula cha saa nne wakati wa kupumzika, na sentensi zinazokuwepo ni, "John you r my friend no? You vill stay with me during mandomando?" Hapo unakubali au unamuuliza atakulipa shilingi ngapi, mara nyingi malipo yalikuwa uhakika wa kuletewa Comics mwezi au kupewa pesa za kwenda sinema kwa kazi hiyo ya ubodigad. Urafiki huo ulikuwa wa muda tu. Pamoja na kuwa katika shule za wahindi kwa miaka mingi nina rafiki wawili tu wa kipindi hicho. Ni ukweli usiopingika kuwa shule nilizotoka zilikuwa na nidhamu ya juu kuliko hizi za Aga Khan, japo huku mambo mengi yalikuwa bora, vitabu, madaftari, maktaba ya shule vilikuweko, kazi kama za kusafisha vyoo huku zilikuwa na mtu maalumu, si zamu za wanafunzi kama nilikotoka. Adhabu zake zilikuwa laini laini, ukikorofisha sana unapumzishwa shule wiki, au adhabu iliyoonekana kali ilikuwa kuandika kosa lako mara nyingi. Ukikutwa unakula Bazooka , basi utaambiwa uandike 'Sitakula bazooka darasani,' mara mia mbili. Unajikuta sentensi hiyo umejaza daftari nzima.
Mambo mengine yalikuwa sawa ngumi za siku ya kufunga shule zilikuweko, na watemi walikuweko, alikuweko kijana moja anaitwa Moez K, yeye ndo alikuwa mtemi mpaka kaka zake walikuwa wanamfwata akawatetee kukiwa na ngumi. Peke yake alikuwa na jeuri ya kutandikana ngumi na waswahili.
Kila asubuhi kabla ya kuingia darasani kulikuwa nakusali, kihindi kwenye foleni haikuchukua muda mrefu wote tulikuwa tunasali kihindi, na hata kuongea kihindi.

Monday, April 5, 2010

Aga Khan Primary



Kutokana na baba kuhamia Mbeya nilihama kutoka Consolata Iringa na kuendelea na shule Aga Khan primary Mbeya, na baada ya mwaka nilirudi tena Iringa ambapo niliendelea kusoma Aga khan primary Iringa. Kuna mambo mengi yalinikuta wakati huu, kwanza shule hizi zilikuwa na asilimia kubwa ya wanafunzi na waalimu wa kihindi, masomo yote yalikuwa ya kiingereza na mimi nilitoka shule ya kiswahili full time. Kiingereza chenyewe cha kihindi. Kwa miezi ya kwanza nadhani nilikuwa nahudhuria tu darasani. Lakini nakumbuka kitu cha kwanza nilichoshangaa ni jinsi watot wa kihindi walivyopenda kula, kila mmoja alikuwa anakuja shuleni na kopo la chakula, wakati wa mapumziko ilikuwa wakati wa kukaa vikundi kila mtu anatoa chakula chake na kajipati kanaendelea. Kila mtu alionekana anakuja shuleni na pesa. Hapa ndio nikakutana na magazeti yanaitwa comics. Beano, Dandy, Beezer, Xmen, Superman, Batman na kadhalika. Kila jumanne Beano na Dandy jipya lilitoka, na kila alhamisi Beezer. Ujio wa magazeti ya Film na Boom yaliongeza utamu na kila Jumanne watu tuliwahi Bookshop kununua Film ili tujue mkasa gani mpya umemkuta Rabon Zoro kwenye mikono ya Lance Spearman. Na Fearless Fang na mikasa yake porini. Kila saa sita magari kibao yalikuwa yanakuja shuleni kuwachukua wanafunzi kuwarudisha nyumbani kwa chakula cha mchana. Vijana wawili walikuwa wanabishana kuhusu uwezo wa Spear kuruka kutoka kwenye magari yanayokimbia kama walivyokuwa wakimwona kwenye picha za magazeti. Mmoja akasema anaweza, na wakati wako karibu na msikiti wa Miyomboni mtoto wa kihindi akajitosa toka kwenye gari, hakupata nafasi ya kuanguka kama Spear, aliangukia uso kwenye lami na kukaa hospitali mwezi mzima

Consolata Primary School 4

Kila shule yenye hadhi enzi hizo ililazimika kuwa na bendi ya shule. Bendi ilipiga kila asubuhi wakati wa ukaguzi. Wanafunzi walikaguliwa kuanzia nywele, kucha nguo meno kama wamepiga mswaki, na siku nyingine kila mtu alilazimika kuja na mswaki kuuonyesha , ole wako uje na mswaki wa kisasa ni viboko tu, ilikuwa lazima utumie mswaki wa mti tena mti maalumu, sababu ilikuwa miswaki ya miti ina utomvu unaotunza meno, miswaki ya plastic lazima uweke dawa. Sweta ilikuwa marufuku, viatu vya ngozi vilikuwa ni nadra sana na anaevaa kulikuwa naina maalumu ya viatu. Bata shoes. Mwenye nywele ndefu alikuwa ananyolewa alama ya msalaba kichwani hivyo mwenyewe anaenda malizia zilizobaki. Wakati wa inspection ulipigwa wimbo wa Baba Paka, au Tanganyika Tanganyika. Kisha nyimbo kama Ngo ngo ngo twaingilia zilikuwa ni za kuingilia darasani. Siku za sherehe ndipo kila shule ilitanguliwa na bendi yake wanafunzi wakienda kwa gwaride safi kuliko mgambo wa siku hizi. Sijisifu lakini bendi yetu chini ya Mwalimu Daudi Luhanga ilikuwa the best wakati huo. Mbwembwe za mshika fimbo ilikuwa ni kivutio tosha huku akiwa kavishwa vitambaa vyenye rangi mbalimbali......loh

Sunday, April 4, 2010

Consolata Primary School 3

Bado mpaka leo najaribu kupeleleza maneno halisi ya wimbo fulani tuliofundishwa na waalimu wa mazoezi wakati huo nikiwa darasa la nne. Tuliambiwa ni wimbo wa kiingereza tuliuimba hivi
My way, may way is cloudy my way God send ze chelenjez down
zea iz fire in ze east and fire in ze west
fire in ze chelenjez da
For God has sent his chelenjez down, God sent his chelenjez down, my lovely

Siku nikigundua mwalimu alitufundisha nini nitafurahi sana. Jumapili ililazimu kuja misa ya pili na baada ya hapo kuripoti shuleni kuitwa majina na kufundishwa nyimbo mpya, ole wako usije utakumbana na mwalimu Daudi Jumatatu. Kwa hiyo kulikuweko na zamu za kutumikia kanisani, wengine kwenda kuuza magazeti ya Kiongozi na Mwenge nje ya kanisa nk.Siku ya kufunga shule, hasa mwisho wa mwaka ilikuwa na sura nyingi sana. Shule nzima na wazazi wenu mnakusanyika yanaanza kutajwa majina ya wanaopanda darasa. Mwalimu wa darasa anasimama na karatasi na kuanza kusoma, "Hawa ndio wanapanda darasa tutasoma kufuatia maksi zao, wa kwanza Naboth Mbembati(siku hizi Doctor Muhimbili)", watu wote heeeeeeeeeeeeeeeeeeee, "Wa pili Emmanuel Mkusa(Yuko Namibia bingwa wa mahesabu huyo)"...watu wote heeeeeeeeeeeeeeeeeeee. Itaendelea mpaka kufika na hawa ndio walioobunda..haya wasimame wanatajwa majina na kuzomewa yuuuuuuuuuuuuuuuuuu. Hapo sasa bado kipigo cha wazazi kinakungojea na kejelei ya shule nzima kwa likizo nzima na mwaka mzima unaofuatia kwa kuwa darasa la nyuma. Mwalimu Mkuu akitangaza shule imefungwa, kulikuwa nambo mengi yanatokea, kulikuweko na watu wanakimbia haraka toka eneo la shule, siku hii ilikuwa ya malipo, ngumi zilikuwa zinaumuka kila kona, huyu anadaiwa gololi, yule hajalipa mikusu , mwingine alimnyima mwenzie kashata. Basi ukisikia 'Ngumi ngumi" unakimbilia kuona kuna nini na siku hiyo haziamuliwi mpaka atandikwe mtu. Likizo ilikuwa raha sana mambo mengi ya kufanya,kutengeneza baiskeli za miti, magari ya maberingi, kwenda Itamba kuiba maembe, kuwinda vindege na manati, na hii ilikuwa kwanza ukisha tengeneza manati yako unafanya chini juu umpige mbayuwayu, halafu unajichanja kisha unapaka damu yake ilijulikana hiyo inakufanya uwe na shabaha sana. Pamoja na kula matunda mengi ya porini na vindege siku ya bahati mnapata sungura ililazimika uweke nafasi ya kula nyumbani kwa sababu ole wako ufike nyumbani useme umeshiba , ikijulikana ulikula kwa watu ni kipigo tu.

Consolata Primary School 2

Waalimu kipindi hicho walihakikisha sheria zinafuatwa haswa, na kiboko kilitembea haraka sana kwa wakorofi. Mwanafunzi aliyekuwa na nguvu kuliko wote hapo shuleni aliitwa Odongo, na huyo ndiye aliyekuwa na kazi ya kuwafukuza wale ambao walikuwa wakikimbia adhabu. Siku moja kundi la wanafunzi walipanga kumuua mwalimu mmoja aliyekuwa na sifa ya ukali sana. Mmoja wa wanafunzi alikuwa ametuhadithia kuwa bibi yake kamwambia kuwa ukikaanga mchanga wa unyao wa mtu anakufa. Msako wa mchanga wa unyao wa mwalimu ulianza. Wakati huo eneo lote la shule mpaka kanisani palikuwa pamemwagwa kokoto hivyo ikawa ngumu kupata unyayo wa mwalimu. Bahati mbaya zaid mwanafunzi mmoja akapata uwoga akamtaarifu mwalimu kuhusu mpango huo wa 'muder'. Loh wakati tuko katikati ya kipindi kengele ikalia shule nzima tukaambiwa foleeeeni. Tukiwa mbele ya shule wakaanza kuitwa majina wote walioshiriki katika kupanga hiyo masta plani. Wote wakatandikwa viboko halafu mwalimu akawapa mchanga wenye unyayo wake akawambia sasa wakakaange vizuri.
Kila alhamisi mchana ililazimu kutoroka shule na kwenda stendi ya mabasi ambayo wakati huo iliwa eneo lilipo soko. Soko lilikuweko ule upande unaoangaliana na kanisa la Kilutheli. Hili la huku juu limejengwa ilipokuwa stendi. Siku ya alhamisi mchana kulikuwa na basi la DMT lililokuwa linatoka Malawi, wakati huo kukiitwa Nyasaland. Huko kulikuwa na mganga aliyekuwa akiogopwa sana jina lake Chikanga, yeye alikuwa na sifa ya kuwatoa uchawi wachawi na kisha kuwanyoa. Kazi yetu ilikuwa kuangalia abiria mwenye kipara hapo ni mawe makopo tu, na wengi walikuwa wakikimbilia kituo cha polisi ambacho kipo hapo toka enzi za ukoloni.

Consolata Primary School

Barabara Mbili
Jiwe la adhabu nje ya shule ya Chemchem
Katika kipindi nilipokuwa nasoma, Consolata aka Chemchem, eneo lote linaloitwa Frelimo lilikuwa pori tu, palikuwa na njia ya mkato toka hapo shuleni mpaka Makorongoni. Nilikuwa nikiishi Barabara Mbili kwenye nyumba ambayo kwa sasa ni kilabu cha pombe. Wakati huo kulikuwa na wenzetu wanakaa Nduli ambao nao walikuwa wanawahi kila siku kuja shule asubuhi saa moja na nusu.Ukichelewa prefect alikuwa anaandika majina, prefect mmoja ambaye sasa ni mkuu fulani, alikuwa bingwa wa kupokea hongo yamatunda kama mitoo, misasati, na mifudu na mahindi ya kuchoma ili asikuandike jina ikiwa umechelewa. Moja ya adhabu mbaya ilikuwa ni kupewa nyundo na kuligonga jiwe lililopo kwenye uwanja wa shule, mwalimu alitakiwa awe anasikia akiwa darasani, kwa kawaida baada ya kugonga dakika kumi ilikuwa kama unajigonga ndani ya kichwa. Kati ya starehe za wakati huo ilikuwa ni kuogelea katika kisima kilichokuwa kwenye makutano ya barabara itokayo stendi na ile iendayo Ilala, wakati huo hapo ilipo stendi palikuwa ni makaburi tu. Starehe nyingine ilikuwa ni kutengeza bunduki zilizoitwa Nyongamembe, au kuteremka Ruaha kwa ajili ya kuchuma mitoo,misasati na mifudu na kuogelea kuvua samaki na kutengeneza kamba za katani kwa kuzileta shule kwenye kipindi cha Maarifa ya Nyumbani. Adhabu ya kufungiwa darasa zima kutokwenda kula mchana nayo ilikuwa maarufu sana.
Nakumbuka hapo mtaani barabara mbili tulianzisha bendi kama zile za shule kwa kuwamba ngoma sisi wenyewe. Ila tuliwahi kuibiwa ngozi na mwalimu mmoja wa shule ya chini ya mti ambaye wote tulikuwa tunamuogopa kwani aliwahi kujaribu kujinyonga chooni kamba ikakatika akawa kama zezeta fulani lakini hiyo shule ya chini ya mti imekuwa shule maarufu mpaka leo.

Hapo zamani za kale 2

Madirisha matatu ya kwanza ni darasa la 1A na 1B

Raha ya shule enzi hizo kwanza ni hadithi za kutisha kama zile za mazimwi, mbwa mwitu, na ujanja wa sungura. Hakuna kusahau jinsi Wagagagigikoko walivyoweza kunitokea ndotoni. Muda wa kupumzika ,ambao pale Chechem ulijulikana kama pausi (pause????) ulitawaliwa na kila aina ya michezo kama vile 'mbinga, gololi, kiboleni, mdako... huku biashara ya misasati, mifudu, mafulusadi zikiendelea.
kulikuwa natatizo moja pale Mlandege, kile choo cha wasichana tuliambiwa kina jini, na ilikuwa lazima uvuke hapo kwenda choo cha wavulana, na kumbuka wakati huo nyuma ya choo cha wavulana kulikuwa na pori kubwa si leo ambapo kumezungukwa na nyumba. Dawa ilikuwa kujitahidi usilazimike kwenda chooni wakati wa vipindi maana utakuwa nje peke yako na jini. Choo cha mbele ni cha wasichana na nyuma ni cha wavulana
Watu wengi waliamua kukojoa darasani kuliko kukutana na jini

Hapo zamani za kale

Nimezaliwa Iringa, wazazi wangu wote walikuwa waalimu. Baba alikuwa akifundisha Iringa Middle School, (iliyoitwa baadae Mshindo Primary School), ambayo wenye akili fulani katika miaka ya sabini, waliamua ivunjwe ili ujengwe uwanja wa Samora. Ilikuwa ndio shule inayofuata baada ya mwanafunzi kumaliza Government Primary School, inayoitwa sasa Mlandege Primary School. Goverment iliishia darasa la nne, na Middle School ilianza darasa la tano hadi la nane. Mama alikuwa mama mendeleo na baadae akafundisha Aga Khan primary,(Shabaha Primary ambayo nayo haipo tena majengo yake yamechukuliwa na Lugalo sekondari). Na pia alifundisha St Mary's secondary , ambayo sasa ni Iringa Girls.
Nakumbuka kuanza shule Mlandege darasa la kwanza ambapo madarasa yalikuwa na makundi mawili 1A, na 1B. Nilikuwa 1B mwalimu wetu alikuwa Mwalimu Chitigo, wakati 1A walikuwa wanafundishwa na Mwalimu Mary. Mwalimu Mkuu alikuwa mwalimu George Nyakunga, ambaye bahati mbaya alifariki mapema miaka hiyo hiyo. Namkumbuka Mwalim George akituita na kutugawia uniform zetu ambazo siku hizo zilikuwa zinashonwa na fundi maalumu wa shule. Kisha nikahamia Consolata Primary ambayo leo inaitwa Chemchem, nikakutana na mwalimu Daudi Luhanga, Mwalimu Kalinga, Mwalimu Filangali, Mwalimu Mkuu akiwa Mwalimu Mwinuka. Kwa kipindi cha mwaka baba alihamia Mbeya nikasoma Aga Khan Mbeya, kisha kurudi Iringa ambapo nilisoma Aga Khan Primary wakiwemo waalim kama Mrs Saleh ambaye hadi sasa anaendesha mgahawa unaitwa Hasty Tasty, mwalim Daya, mwalimu Pabani, mwalimu mkuu akiwa Mr Thakore, kisha nilijiunga Aga Khan Secondary chini ya mwalimu Mkuu Mr Sheikh na baadae Mr Ntemo, na Mr Hassan, mwisho Iringa Teachers training Centre- Klerruu College of National Education., hapa Principal alikuwa Mzee Basimaki, ambae baadae alifuatiwa na Mr Kilimuhana. Wakufunzi wengi wa hapa walipanda sana katika serikali kuu. Mr Halinga aliwahi kuwa Mbunge Mbozi, Mr Mwanga alikuja kuwa Waziri wa Utumishi, Mh Ngw’andu waziri wa Sayansi na Technolojia.


STAT COUNTER