Pages

Sunday, April 4, 2010

Consolata Primary School 3

Bado mpaka leo najaribu kupeleleza maneno halisi ya wimbo fulani tuliofundishwa na waalimu wa mazoezi wakati huo nikiwa darasa la nne. Tuliambiwa ni wimbo wa kiingereza tuliuimba hivi
My way, may way is cloudy my way God send ze chelenjez down
zea iz fire in ze east and fire in ze west
fire in ze chelenjez da
For God has sent his chelenjez down, God sent his chelenjez down, my lovely

Siku nikigundua mwalimu alitufundisha nini nitafurahi sana. Jumapili ililazimu kuja misa ya pili na baada ya hapo kuripoti shuleni kuitwa majina na kufundishwa nyimbo mpya, ole wako usije utakumbana na mwalimu Daudi Jumatatu. Kwa hiyo kulikuweko na zamu za kutumikia kanisani, wengine kwenda kuuza magazeti ya Kiongozi na Mwenge nje ya kanisa nk.Siku ya kufunga shule, hasa mwisho wa mwaka ilikuwa na sura nyingi sana. Shule nzima na wazazi wenu mnakusanyika yanaanza kutajwa majina ya wanaopanda darasa. Mwalimu wa darasa anasimama na karatasi na kuanza kusoma, "Hawa ndio wanapanda darasa tutasoma kufuatia maksi zao, wa kwanza Naboth Mbembati(siku hizi Doctor Muhimbili)", watu wote heeeeeeeeeeeeeeeeeeee, "Wa pili Emmanuel Mkusa(Yuko Namibia bingwa wa mahesabu huyo)"...watu wote heeeeeeeeeeeeeeeeeeee. Itaendelea mpaka kufika na hawa ndio walioobunda..haya wasimame wanatajwa majina na kuzomewa yuuuuuuuuuuuuuuuuuu. Hapo sasa bado kipigo cha wazazi kinakungojea na kejelei ya shule nzima kwa likizo nzima na mwaka mzima unaofuatia kwa kuwa darasa la nyuma. Mwalimu Mkuu akitangaza shule imefungwa, kulikuwa nambo mengi yanatokea, kulikuweko na watu wanakimbia haraka toka eneo la shule, siku hii ilikuwa ya malipo, ngumi zilikuwa zinaumuka kila kona, huyu anadaiwa gololi, yule hajalipa mikusu , mwingine alimnyima mwenzie kashata. Basi ukisikia 'Ngumi ngumi" unakimbilia kuona kuna nini na siku hiyo haziamuliwi mpaka atandikwe mtu. Likizo ilikuwa raha sana mambo mengi ya kufanya,kutengeneza baiskeli za miti, magari ya maberingi, kwenda Itamba kuiba maembe, kuwinda vindege na manati, na hii ilikuwa kwanza ukisha tengeneza manati yako unafanya chini juu umpige mbayuwayu, halafu unajichanja kisha unapaka damu yake ilijulikana hiyo inakufanya uwe na shabaha sana. Pamoja na kula matunda mengi ya porini na vindege siku ya bahati mnapata sungura ililazimika uweke nafasi ya kula nyumbani kwa sababu ole wako ufike nyumbani useme umeshiba , ikijulikana ulikula kwa watu ni kipigo tu.

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER