Pages

Sunday, April 4, 2010

Consolata Primary School 2

Waalimu kipindi hicho walihakikisha sheria zinafuatwa haswa, na kiboko kilitembea haraka sana kwa wakorofi. Mwanafunzi aliyekuwa na nguvu kuliko wote hapo shuleni aliitwa Odongo, na huyo ndiye aliyekuwa na kazi ya kuwafukuza wale ambao walikuwa wakikimbia adhabu. Siku moja kundi la wanafunzi walipanga kumuua mwalimu mmoja aliyekuwa na sifa ya ukali sana. Mmoja wa wanafunzi alikuwa ametuhadithia kuwa bibi yake kamwambia kuwa ukikaanga mchanga wa unyao wa mtu anakufa. Msako wa mchanga wa unyao wa mwalimu ulianza. Wakati huo eneo lote la shule mpaka kanisani palikuwa pamemwagwa kokoto hivyo ikawa ngumu kupata unyayo wa mwalimu. Bahati mbaya zaid mwanafunzi mmoja akapata uwoga akamtaarifu mwalimu kuhusu mpango huo wa 'muder'. Loh wakati tuko katikati ya kipindi kengele ikalia shule nzima tukaambiwa foleeeeni. Tukiwa mbele ya shule wakaanza kuitwa majina wote walioshiriki katika kupanga hiyo masta plani. Wote wakatandikwa viboko halafu mwalimu akawapa mchanga wenye unyayo wake akawambia sasa wakakaange vizuri.
Kila alhamisi mchana ililazimu kutoroka shule na kwenda stendi ya mabasi ambayo wakati huo iliwa eneo lilipo soko. Soko lilikuweko ule upande unaoangaliana na kanisa la Kilutheli. Hili la huku juu limejengwa ilipokuwa stendi. Siku ya alhamisi mchana kulikuwa na basi la DMT lililokuwa linatoka Malawi, wakati huo kukiitwa Nyasaland. Huko kulikuwa na mganga aliyekuwa akiogopwa sana jina lake Chikanga, yeye alikuwa na sifa ya kuwatoa uchawi wachawi na kisha kuwanyoa. Kazi yetu ilikuwa kuangalia abiria mwenye kipara hapo ni mawe makopo tu, na wengi walikuwa wakikimbilia kituo cha polisi ambacho kipo hapo toka enzi za ukoloni.

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER