Pages

Tuesday, August 16, 2022

KISA CHA MUYOVELA KUKIMBILIA UGOGONI


Mihwela alipofariki, wale watoto wake  wawili wa kiume, Muyoviligombo au Myovela na Mwengamagoha, wakaamua kugawana nchi ya baba yao na kumpa binamu yao Munyigumba mali. Munyigumba akakataa na kudai apewe eneo la kutawala. Ndugu zake wakampuuza, na yeye akajifanya kama pia hana shida kumbe alianza kupanga mipango ya chinichini ya kupata alichokuwa anakitaka. Kwanza akaanza kuonyesha ukaribu mkubwa na  Mwengamagoha, kwa kuwa huyu alikuwa na hasira za harakaharaka akawa anamtumia kumchokoza kaka yake kwa hila moja au nyingine. Alipoona hila zake hazimtii hasira Myovela akaona abadili utaratibu, siku moja akamualika Myovela amtembelee Ng’uluhe, baadhi ya Wadongwe mashuhuri waliompenda Myovela akina Luvanga, Mulala, Nyakunga, wakamkataza asiende, tena wakamshauri kuwa ni heri aondoke na watu wake na mifugo yake na kuhamia nchi nyingine, kwani ni lazima Munyigumba takuja kupiga. Myovela na watu wake wakaondoka na kutembea mpaka Izazi wakataka kuweka masikani pale, lakini wakapata habari kuwa Munyigumba na jeshi lake wanawasaka, wakalazimika kuondoka na kuvuka mto Lyambangali mpaka Ilolo, kule kulikuwa na mtawala aliyeitwa Msane, Msane aliwakaribisha Myovela na watu wake, lakini Myovela hakukaa sana hakutaka wenyeji wake aliyemkaribisha vizuri aje apewe adhabu na Munyigumba kwa ajili yake. Aliendelea na safri hadi Nyamasitu, akapumzika na watu wake pale, lakini tena akaambiwa kuwa adui bado anamfuata. Myovela aliendelea na msafara mpaka jirani na ulipo mji wa Kibakwe siku hizi, eneo hilo lilikuwa likitawaliwa na Mdemu mtoto wa Manyile, huyu aliposikia jeshi la Wadongwe lililoongozwa na Myovela linamkaribia hakungoja, aliondoka na watu wake na kukimbilia Ugogo. Wanyandewela wa Mudemu walikuwa wana haki ya kuliogopa jeshi la Myovela maana habari za ukali wa Wadongwe zilifahamika sana.  Lakini  bahati haikuwa ya Mudemu, jeshi lake  lilipofika karibu na ilipo Mvumi,  likashambuliwa na Wagogo na Wamasai na kuangamizwa karibu lote, mahala pale pakaitwa Makang’wa, na wajukuu wa waliosalimika katika maangamizi yale mpaka leo hutumia kiapo cha Kumakang’wa kukumbuka ilikolala mizimu yao.
Muyovela alitulia kwa miaka kadhaa katika makao yake mapya, watu wake wakaanza kusambaa na kuishi bila woga kwani wenyeji waliwaogopa sana hawa wageni, waliendelea kuishi na hadi leo wakazi wa maeneo ya Wota waliotokana na msafara huo wa Myovela hujitambua kuwa ni Wahehe na hufuata mila zote za Kihehe.

Myovela aliondoka tena na watu wake wengine na kuelekea  Nondwa iliyokuwa katika himaya ya Ugogo, kwenye tambarare  kusini mwa bwawa la Kinyambwa, aliafikiana na wenyeji kule na akaishi kwa raha ukiachia mapigano ya hapa na pale na Wamasai aidha kwa kuwaibia ng’ombe au walipokuwa wakiibiwa ng’ombe.

Huku nyuma Mnyigumba na Mwengamagoha wakaamua kugawana nchi. Munyigumba akamshauri Mwengamagoha akajenge ikulu yake Nzihi, wakati yeye akaendaa kujenga ikulu yake Lungemba. Myovela alipopata habari ya kinachoendelea akatuma ujumbe kwa nduguye na kumsihi  akajenge ikulu yake Luhota kwani ndiko ilikokuwa chanzo cha himaya ya baba yake, angekuwa kati ya watu wake,  Nzihi ilikuwa ni kama ugenini. Mwengamagoha  akampuuza kaka yake. Na kuanza kujenga ikulu yake Nzihi. Munyigumba akatuma kikosi cha siri kikaenda kushambulia Nzihi, mke na watoto wote wa Mwengamagoha waliuwawa, na yeye alinusurika tu  kwa kujificha kwenye shimo lililokuwa linachimbwa udongo wa kujengea ikulu yake.

Mwengamagoha alipopata nafasi akatoroka na kuelekea alikokuwa kaka yake Ugogoni. Alipofika kaka yake alimpokea vizuri lakini alimkaripia sana kwa upumbavu wake wa kutokutambua kuwa Munyigumba alikuwa adui yao wote. Mwengamagoha aliyapokea makaripio ya kaka yake vizuri lakini wake na watoto wa Muyovela waliendelea kumtania na hata kumtungia nyimbo za kejeli, hakuweza kuvumilia akahama na kuelekea Usangu na baadae Ukosikamba  hatimae akafia Udonya akiwa hana nchi,

 

 

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER