Pages

Friday, August 12, 2022

UNAJUA JINSI MUNYIGUMBA ALIVYOPATA JINA LAKE?

 


Mtoto wa kwanza wa Kilonge na Sekindole aliitwa Mugavanalupembe. Huyu ndie aliyerithi utawala wa Ng’uluhe, lakini hakutawala muda mrefu kwani aliuwawa na Muhingile Mwangwenga kwenye ugomvi wakati wa kunywa pombe. Muhingile alitoroka na kujificha kwa muda mrefu lakini alipojitokeza kitu cha ajabu, hakuna aliyemkamata au kumhukumu.
Mtoto wa pili wa Kilonge na Sekindole aliitwa Binini. Jina hili halikupendwa sana na  kwani lilikuwa likitambulisha umbo la mtoto huyu kuwa alikuwa na aina ya kibyongo. Alikuja kujulikana zaidi kwa jina la Munyigumba au Mugohang’amwa yaani Mkuki unakamulika, kwani kwa kutumia mikuki alipata mali kama mtu mwenye ng’ombe anavyokamua maziwa.

Wakati kaka yake Mugavanalupembe alipokuwa akitawala Ng’uluhe, Binini alipelekwa kukulia kwa mjomba wake shujaa Mihwela. Mihwela alikuwa binamu ya Sekindole mama wa Binini hivyo alikuwa mjomba wake. Huko akajifunza mbinu za vita na utawala. Akaanza nae kuwa na hamu ya kutawala.

Mihwela alikuwa na watoto wa kiume wawili, Muyoveligombo na Mwengamagoha. Huyu Muyoveligombo alikuwa mwanamuziki  aliyependa kupiga ‘ligombo’, aina ya gitaa la asili ya Uheheni, na pia kuimba. Na ndivyo alivyopata jina la Muyoveligombo ambalo baadae likafupishwa na kuwa Muyovela. 

Huyu Mwengamagoha alikuwa mtu wa kukasirika kasirika na  mwenye jeuri. Mihwela aliwahi kumkemea mara kadhaa mwanae huyu kutokana kuwa na jeuri. Kuna wakati aliwateka watu wawili, Mwisaka mmoja na Mwachusi mmoja, akawatesa sana na hatimae akamuua yule Mwisaka, Mihwela alikasirika sana na kumwambia mwanae kuwa anafumua misingi ya kuunganisha  koo mbalimbali na hivyo kuwa na nguvu za pamoja na pia kwa kuwa watu hawa walikuwa mashujaa katika mapambano kadhaa aliyofanya Mihwela. Lakini Mihwela alifahamu pia kuwa Binini ndie aliyekuwa akichochea hayo ili apunguze nguvu za kumpinga wakati atakapoanza mbinu zake za kuchukua utawala.
Mihwela alimwambia mwanae Myovela kuwa apigane na Mwengamagoha na Binini wakati akiwa bado na uwezo kwani alikuwa ameota ndoto kuwa  Muyovela alikimbilia nchi ya mbali, kavu na yenye joto nje ya Uhehe. Lakini wajukuu zake watarudi Uhehe ila wakati huo watu weupe watakuwa wamefika na kuchimba ardhi na kujenga vichuguu vikubwa vyeupe. Myovela alikuwa mtu wa amani hakutaka kupigana na ndugu zake, hivyo akapuuza maagizo ya baba yake, lakini miaka mingi baadae ndoto ya baba yake ilitokea kama alivyoiota, kama tutakavyoona hapo baadae.

Wakati Binini yupo Luhota akaoa mke kutoka ukoo wa mwa Ngimba wa Ilole. Akina NGimba asili yao ni Hamitiki hivyo mpaka leo hutokeza wajukuu warefu wenye vidole virefu, masalia ya DNA ya Wahamitiki..
Binini alipoitwa kweda kwenye msiba wa kaka yake Mugavanalupembe alikataa na kusema kuwa angetaka kwanza aende kuwapiga Wasangu, kwani aliamini baada ya hapo angerudi na mali nyingi na utukufu hivyo kuchukua kirahisi himaya iliyokuwa ya kaka yake. Alikusanya vikosi vya Wadongwe wa Luhota na akapata vikosi vingine kutoka kwao Ng’uluhe, na askari wote walitakiwa kukutana Lungemba, Binini mwenyewe alipofika Lungemba,  ndugu zake akina Kindole wakamuongezea askari, akawa na jeshi kubwa. Aliingia Usangu na kuwashambulia ghafla Wasangu na kuteka mali nyingi na wanawake. Binini mwenyewe akamuua kiongozi wa Wasangu aliyeitwa Munyigumba na akatwaa jina lake kama kumbukumbu ya vita hiyo. Baada ya ushindi huo akaanza kurudi Ng’uluhe akapitia Mufindi iliyokuwa chini ya binamu yake Musambila Mwamdemu mtoto wa Chawala. Huyu alitawala Ifwagi, Mufindi na hata sehemu za Malangali. Munyigumba alipokelewa kwa shangwe na ngoma, lakini katikati ya sherehe akamchoma mkuki mwenyeji wake na kumuua na kujitangaza mtawala.  Na nia yake ya kupitia Mufindi ikadhihirika kwani alikuwa kapita ili kulipa kisasi kwani Musambila hakumpa askari wakati anaenda kupigana na Wasangu, na pia kuanza kutimiza ndoto yake ya kutawala eneo kubwa.

 

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER