Pages

Thursday, August 11, 2022

MIHWELA MUHEHE ANASTAHILI KUITWA SHUJAA WA TAIFA

Mihwela azuia utumwa

Katika mfululizo wa historia hii nimeongelea mambo makubwa aliyofanya Mihwela mjukuu wa Chota. Lakini  mtu huyu bahati mbaya jina lake huwa halitajwi sana katika watu muhimu Uheheni, licha ya makubwa aliyowafanyia watu wa Uheheni. Tuliona jinsi alivyokuwa wa kwanza kuanza kuanzisha mpangilio wa mafunzo ya kijeshi kwa askari na alivyoweza kushinda vita kadhaa kiasi cha koo na kabila ndogondogo mbalimbali kuanza kumuita awatawale ili wapate ulinzi wa askari wake. Leo tutazungumzia jambo moja kubwa sana alilolifanywa Mihwela.

Kati ya mwaka 1820 na 1830, Waarabu walianza kuingia bara kutoka pwani na kuanza kuteka watu ili wakauzwe na kuwa watumwa kwenye mashamba ya Karafuu huko Unguja.
Kikosi kimoja cha waarabu kikaingia sehemu za Pawaga na kuteka watu wengi na kuwaweka katika makambi tayari kwa safari ya kwenda pwani kuuzwa Pwani, baadhi ya watu walioweza kutoroka walikimbia na kwenda kumtaarifu Mihwela ambaye alikusanya jeshi lake na kuweza kusafiri na hatimae kufika usiku karibu na kambi hiyo ya Waarabu. Jeshi la Mihwela lilijipanga na kuizunguka kambi ile, mapema alfajiri jeshi lile lilifanya mashambulizi na kuteketeza Waarabu wote, wakamuachia mmoja tu aliambiwa akatoe taarifa kuwa Wadongwe wamepiga marufuku biashara ya utumwa eneo lile.
Na tangu wakati ule biashara ya utumwa uheheni ilikufa, Wahehe wachache walioingia utumwani ni wale waliorubuniwa kuondoka mipaka ya Uheheni na huko kujikuta wakitekwa na kuuzwa. Wanyamwezi wanasemekana  walikuwa maarufu kwa ujanja huu wa kuwa rubuni Wahehe kuondoka katika usalama wa nchi yao.
 Waarabu walikuja baadae kufanya biashara Uheheni lakini si biashara ya utumwa, Ila ieleweke kuwa Wahehe wenyewe walikuwa na watumwa waliofanya kazi mashambani, majumbani na kwenye shughuli za uchungaji.
Kiukweli kwa hili Mihwela alistahili kuwa shujaa si wa Uheheh tu bali wa nchi yetu ya Tanzania.
Kama mnakumbuka babu yake Mihwela, Chota,  alimuua Mnyaluhwao siku ya kwanza ya kukutana nae hivyo kuzuia kuja kupingwa baadae, na Mihwela alitumia akili hiyohiyo kuzuia upinzani pale alipohisi unaweza kuja kutokea, himaya yake ikaanza kukua.
Kama tulivyoona awali alimaliza uasi wa Wasawila kwa kuwapiga wasaidizi wao Wasangu, akawaweka chini ya utawala wake Vanyandevelwa waliokuwa chini ya mtawala wao Mdemu mtoto wa Manyile ambaye baada ya mapigano kadhaa alikimbilia Wota.

Wahehe 

Jeshi la Mihwela lilikuwa na vikosi

Jeshi la Mihwela lilikuwa na vikosi vyenye watu 200 kila kikosi. Taratibu hii ya kuwa na askari 200 kila kikosi inaonekana ilikuwa ya kawaida katika Afrika, kwani miaka mingi kabla ya hapo Vanyangologo walipoingia Uheheni walikuwa wakitembea kwa vikosi vya watu mia mbili mia mbili, hata Shaka wa Wazulu jeshi lake pia lilikuwa na mfumo huo, na hata Mkwawa baadae alikuwa na jeshi lenye vikosi vya idadi hiyohiyo.

Wadongwe walipenda sana mtindo wa kuwazunguka adui usiku na kisha kuwashambulia alfajiri mapema, kila askari wa Wadongwe alikuwa na ngao iliyotengenezwa kwa ngozi ya ng’ombe iliyokuwa na urefu wa kwenda juu kimo cha askari na upana wake kiasi cha upana wa binadamu. Pia kila askari alikuwa na mikuki miwili, mmoja mwembamba alioutupa na mwingine wenye bapa nene, ulioitwa lisala, ulitumika kuchoma adui na kuchomoa kama kisu.
Mdongwe alikuwa akipigana na adui mwenye mkuki alisimamisha ngao yake, na kama ni adui waliotumia visu na mapanga kama Wahuma ngao aliishika kwa kuilaza upande kusudi kisu kisichane ngao ile kutoka juu mpaka chini. Kuna hadithi kuwa Wahehe walianza kutumia ngao baada ya kupigana na Wangoni, hii si kweli Wategeta walianza kutumia ngao baada ya mapigano yao na Wahumma na kuona Wahumma walivyofaidika na kinga hiyo

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER