Pages

Sunday, August 21, 2022

MKWAVA ALIPOIKIMBIA NCHI YA BABA YAKE

 


Baada ya Shaka ka Senzangakhona, au kwa jina maarufu Shaka Zulu,kurithi utawala wa Wazulu baada ya kifo cha baba yake, kati ya  mwaka 1818 na 1828 alianzisha utawala wa kikatili wa kuua na kuteka tawala zilizokuwa jirani yake. Kipindi hiki kigumu kwa Wazulu kilipewa jina Mfecane, viongozi wa makabila makubwa kama Zwangendaba, Mzilikazi, na  Shoshangane wakaanza kuhamisha watu wao na kuelekea kaskazini mwa nchi yao ya awali ili kukimbia vita hizo za Shaka Zulu, nao katika kusafiri kwao wakapiga na kuteka mali za makabila walioyakuta njiani mwao bila huruma. 
Wavamizi hawa wengine wakaingia eneo sasa linaloitwa Tanzania kupitia iliko Malawi, wengine wakabaki sehemu ulipo mkoa wa Ruvuma hawa wakaja julikana kwa jina la Wangoni, jina lililokuwa kwa asili  la ujumla wa makabila mengi yaliyokuwa jirani na Wazulu.  Baada ya kutujila na kujijenga sehemu hii, mwaka 1878 jeshi la Wangoni lilipenya Ubena toka kusini mpaka kaskazini bila upinzani wowote na hatimae kuingia katika himaya ya Munyigumba.
Askari wa jeshi hili la Wangoni, walikuwa hodari wasioogopa kifo. Walitumia bangi kuondoa hofu yoyote, hivyo walifanya walichotaka katika nchi ya Ubena.
Munyigumba alikuwa hajapata nafasi ya kutayarisha majeshi yake kwa uvamizi wa watu hawa kutoka kusini,  hivyo alipojaribu kuwazuia  kazi ilikuwa ngumu sana, majeshi ya Munyigumba yalianza kusukumwa nyuma kwa urahisi kabisa. Munyigumba alirudishwa nyuma hadi karibu na Image na akalazimika kukimbilia kwenye mapango ya Nyamulenge na kujificha humo. Wangoni walipomgundua walimzingira na hakika ilionekana kuwa ndio mwisho wa Mutwa huyo.

Bahati nzuri sana  mwanae Munyigumba, Mukwava aliyekuwa na umri wa miaka 23 wakati huo alikuwa tayari askari jemadari aliyekamilika, hivyo alikusanya askari na kutengeneza jeshi imara na kuelekea Image. Alijipanga vizuri na kuwazunguka Wangoni, kisha kuwashambulia kutoka mgongoni, Wangoni hawakuwa na namna ila kujiokoa, wakakimbia wakirudi kwao kupitia Lulanga, kule wakashambuliwa tena na Mutengela aliyekuwa mutwa wa Wakinamanga, tena yeye akawafukuza mpaka ndani ya nchi yao.  Wangoni hawakuamini kipigo hicho kwani katika vita zao zote walikuwa na kawaida moja tu kushinda vita. Walirudi kwao na kutulia kwa muda mrefu.

Kiasi cha mwaka mmoja baada ya mapambano hayo na Wangoni, Mutwa Munyigumba akafariki.

Kikaanza kipindi chenye mashaka sana, kwani wakati wa uhai wake Munyigumba alikuwa na msaidizi wake ambaye alikuwa pia mkwewe. Mtu huyu aliyekuwa pande la mtu na ambaye Munyigumba alimpa mamlaka makubwa, hivyo  alikuwa akihofiwa sana. Huyu bwana alikuwa wa ukoo wa Lunyungu, kwa majina alikuwa akiitwa Mwanakimamule au Pokavilonga. Mwenyewe alijiita wa ukoo wa Mwamubambe au wengine huita Mwambambe, jina alilolitoa kutoka jina la baba yake Mubambe.
Wakina pia Muyinga walimhofu sana mtu huyu na hofu yao haikuwa bure hakuwa mtu wa kawaida. Kutokana na hofu hiyo akina Muyinga wakaacha kumtawaza Mkwava kwa vile waliona bado kijana mdogo ambaye walihisi asingeweza kushindana na hila za Mwamubambe. Hivyo wakamteua ndugu yake aliyeitwa Mhalwike awe Mutwa.  Haikuchukua muda mrefu woga wa kina Muyinga ukadhihirika,  Mwamubambe alimuua Muhalwike na kumtawaza ndugu yake aliyeitwa Mwamuhenga. Huyu alikuwa mtawala jina tu kwani mtawala rasmi alikuwa Mwamubambe.
Hapo ikalazimika Mkwawa aikimbie nchi yake mwenyewe.

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER