Pages

Monday, August 29, 2022

MKWAVA APOKELEWA NA MUYOVELA UGOGONI

 


Mukwava inasemekana alizaliwa Luhota kwenye mwaka 1855. Alipokuwa mdogo aliitwa Ntasalatsi, yaani mtu mwenye kupapasa kwa mikono na vidole anapotafuta kitu. Mkwava aliishi kwenye nyumba iliyokuwa haikosi simulizi za ushujaa wa baba yake na askari wake. Akiwa bado mdogo baba yake, Mutwa Munyigumba, alikwenda kuwa kuwapiga Wasangu na kupanua utawala wake mpaka Ng’uluhe.
Mutwa Mihwela alipokufa, mtawala ambaye alikuwa mjomba wa Muyingumba na aliwahi kumlea kwa muda mrefu,   Muyigumba alifanya kila hila mpaka binamu yake Myovela akalazimika kukimbia himaya yake na kwenda kujificha Ugogoni, na Munyigumba aliweza kuiteka kirahisi himaya hiyo na ikawa chini yake, na baadae akaweza kumnyan'ganya himaya binamu yake mwingine Mwengamagoha, mdogo wake Myovela, ambaye naye alilazimika kukimbilia alikokuwa kaka yake. Munyigumba akaweza kuunganisha koo ndogondogo nyingi kuwa chini yake na hakika alikuwa ni muhimili mwingine katika ujenzi wa kabila la Wahehe.

Munyigumba akaweka  Ivaha(ikulu) yake Muhana  sehemu iliyoka jirani na Luhota, na huko ndiko kulikuwa na kambi ya kuwazoesha vijana wa jeshi lake mbinu za vita. Kwa vile utawala wake ulipanuka sana, Munyigumba akaweka watu wake waaminifu kuwa viongozi kwenye sehemu mbalimbali alizokuwa akizitawala. Viongozi hawa waliitwa Vanzagila. Hawa pia walikuwa viongozi wa jeshi lililokuwa chini yao ambalo Mutwa angeweza kuwaita wakati wowote.

Kati ya mateka wa vita za Muyigumba alikuweko mateka mmoja wa Kinyamwezi, mateka huyu alikuwa mtoto. Mateka huyu alianza kutumiwa kwa kutumwa kubeba dawa za zilizoaminika kuwa ndizo zilikuwa za kulinda ukubwa, akaanza kuaminika na kupendwa sana na Munyigumba. Pamoja na ushauri aliopewa na wazee kuhusu kujihadhari na mapendo na madaraka makubwa aliyokuwa akimpa mtu huyu, Munyigumba aliongeza tena kwa kumwozesha mtu huyu binti yake. Mtu huyu aliitwa Mwanakimamule, ila jina lake lililokuja kuwa maarufu lilikuwa Mwamubambe au Mwambambe.

Mwambambe alikuwa jitu la miraba minne lenye nguvu sana, inadaiwa vitani alikuwa akitangulia mbele na yeye alikuwa anawakamata adui kwa mikono yake na kuwavunja kisha kuwatupa nyuma yake wamalizwe na askari waliokuwa wakimfuata.  Inasemekana katika kuwa mtumwa wa kubeba madawa ya Munyigumba na yeye alitumia madawa hayo ya mizimu hivyo ikawa si rahisi kumuua.  Katika ile vita ambapo Wangoni walimzingira Muyugumba na jeshi lake katika mapango ya Nyamulenge, Mwamubambe na Mkwawa walikuwa bega kwa bega walipoenda kumuokoa Munyigumba. Kiasi cha mwaka mmoja baada ya kuokolewa kutoka kwa Wangoni, Mutwa Muyigumba akafariki.
Na bada ya muda kukatakiwa kuchaguliwe mtu wa kumrithi.  Wazee wa ukoo wa  Muyinga wakaingia katika wakati mgumu wa kuchagua mtu sahihi kwani walijua wazi kuwa Mwamubambe angewasumbua, hivyo wakawa wanatafakari nani angeweza kutawala na kuweza kumdhibiti Mwamubambe ambae alikuwa na nguvu nyingi pamoja ya kuwa hakuwa mwenyeji. Hatimae wakamteua Muhalwike arithi kiti cha Munyigumba,  haikuchukua muda  Mwamubambe alimuua Muhalwike, na wengine husema alishawishiwa na mkewe mtoto wa Munyigumba. Mwamubambe akamtawaza ndugu yake mmoja aliyeitwa Muhenga kutawala himaya ya Muyigumba, huyu Muhenga alikuwa mtawala jina tu kwani Mwamubambe ndie aliyetawala haswa. Watoto wengine kadhaa wa Muyigumba waliendelea kuuwawa na Mwamubambe, kwa usalama wake Mkwava akalazimika kuimbia himaya iliyokuwa ya baba yake.
Kitu cha ajabu akalazimika kukimbilia  Nondwa Ugogoni kwa mjomba Muyovela. Ikumbukwe kuwa Muyovela alikimbilia Nondwa kwa kufukuzwa na Muyigumba baba yake Mkwava. Ila ni wazi Mkwava alijua kuwa Myovela hakuwa mtu wa visasi, kwani hata mdogo wake Mwengamagoha aliwahi kumsaliti na kujiunga na Muyigumba lakini mambo yalipomuharibikia alikimbilia kwa kaka yake Myovela na akapokelewa bila kinyongo.
Ilikuwa katika wakati wa msafara huu wa kukimbilia Ugogo ambapo inadaiwa mama yake Mukwava, Sengimba, alijitupa kwenye mto sehemu iliyoitwa Kikongoma. Katika sehemu hii mto unapita chini ya ardhi, wenyeji hupaita hapo Daraja la Mungu.
Kuna hadithi mbalimbali kuhusu tukio hilo. Kuna wanaosema mama huyo alikuwa kwenye msafara wa Mwanawe wakielekea Ugogoni ndipo alipoamua kujitosa  kwani hakutaka kuendelea na safari na hakutaka kutekwa na Mwamubambe. Kuna hadithi nyingine za wazee wanasema mama huyo alitekwa na Mwamubambe akawa anadaiwa akaonyeshe zilipo dawa zilizokuwa zikimfanya mumewe Muyingumba kuweza kutawala, hivyo aliwaelekeza kuwa zipo hapo Kikongoma, lakini walipofika aliwaambia kuwa dawa hizo hazitakiwi kuonekana na wanaume hivyo apewe wanawake wa kumsindikiza kuzifuata, na ndipo alipofika kwenye daraja hilo akajitosa mtoni na kujiua.

Msafara wa Mkwava ulipofika jirani na Nondwa, ujumbe ulitumwa kwenda kuomba hifadhi, Muyovela hakuwa na kipingamizi lakini mtoto wake,  Mubogamasoli, hakutaka kabisa kusikia habari za Mkwava, kwanza alikumbusha jinsi baba yake Mkwava alivyowanyang’anya nchi, pili Mubogamasoli alikuwa na uchungu wa kunyang’anywa mpenzi wake na Mkwava. Kabla ya kukimbilia Nondwa, Mubogamasoli alikuwa kamchumbia Semsilamugunda, lakini alipoondoka huku nyuma Mkwava akamuoa Semsilamugunda, ambaye ndiye alikuja kuwa mama  wa mwanae wa kwanza Sapi, baba ya Mutwa Adam Sapi.

Ili kumtuliza mwanawe, Muyovela akamuahidi kuwa Mkwava hataletwa Nondwa, akatuma watu wakamchukua Mukwava na kumpeleka Nzuguni, Muboga masoli akatulia.
Nae  Mkwava alipofika Nzuguni akaanza kupanga namna ya kurudi kwao kwenda kuchukua himaya ya baba yake

   

 

2 comments:

STAT COUNTER