Pages

Tuesday, August 2, 2022

JE UNAJUA CHANZO CHA USEMI 'LUSUNGU LWA MNYALUHWAHO'?



Baada ya vurugu ya Vanyangologo kwisha, nchi ya Uhehe ikatulia kwa muda na ikaendelea kupata wageni kutoka sehemu nyingine mbalimbali, waliokuja kuhamia Uheheni.  Kutoka Ukimbu yalikuja makundi mawili, moja likiongozwa na Ndondole na Muntsali na la pili liliongozwa na Mwigiha na Nyilowa. Kutokana na maelezo ya wahenga, watu hawa hawakuwa weusi,  walikuwa weupe japokuwa weupe wao si ule wa wazungu.

Kundi la Ndondole na Muntsali likaja kuhamia panapoitwa Panunu karibu na lilipo kanisa Katoliki la Malangali, na kundi la Mwigiha na Nyilowa likaenda kuweka maskani yake Uhafiwa. Kuna uwezekano mkubwa kuwa makundi haya yalikuwa na chanzo kimoja kwani mwiko wa kundi la Mwigiha na Nyilowa, ulikuwa ni ule ule wa kundi la Muntsali na Ndondole , mwiko wao ulikuwa ng’anga au  Kanga. Pia hata mwidikiso wao wote ulikuwa Nyamahuvi. Baadae Nyilowa  aliongoza kundi lake na kwenda kufanya maskani yao Lutemi na kule Makungu. Kati ya watoto wote wa Nyilowa, aliyekuja kuwa maarufu zaidi ni Nyakunga.  Watoto wa Mwigiha walikuja kuwa watawala., mtoto wake wa kwanza aliitwa Lyelu, huyu  alitawala kuanzia Welu hadi Pawaga, na mtoto wake  mwingine aliitwa  Mwano, huyu  alitawala kuanzia kilima cha Utinde, kaskazini mwa Kalenga, sehemu ya ilipo Iringa sasa na mpaka  sehemu za Nduli, na  sehemu kadhaa za Pawaga mpaka Manyile juu ya Ndewela.  Kuna akina Nyakunga mpaka karibuni wamekuwa wakizaliwa na kuwa na nywele nyekundu au zenye rangi ya dhahabu. Na kuna wajukuu wa akina Mwano walio na nywele za singa laini za kahawia, za kukaribiana na rangi za nywele za wazungu.
Muntsali alikuja kuongoza wafuasi wake wakahamia Wanging’ombe, huko akawa mtawala. Mwanamke mmoja kutoka ukoo wake alikuja kuolewa Uwanji na mwanae ndie akaja kuwa Chifu Merere wa kwanza aliyetawala, huyu aliwatawala Wasangu na Wasafwa.
Jina la awali la Ndondole lilikuwa Benna, siku hizi wajukuu wanaume wa ukoo huitwa kwa mwidikiso wa Benaa na wanawake Nyatende. Ndondole pia alikuwa na watoto wengi lakini waliokuja kujitokeza zaidi katika historia ya Wahehe ni Chavala na Kimamu.
Chavala alikuja kuhamia Mufindi, na ukoo uliokuwa unatawala kule, ukoo wa Kavindikadodi, ukamuachia nchi atawale. Akapata mke Sekiduku, ambaye alipata mimba lakini wakati wakati wa kuzaa mtoto akawa hatoki, hivyo wakalazimika kufanya kile ambacho ni cha kawaida siku hizi, nacho ni kutanua njia kwa kumchana, na mtoto akazaliwa salama. Kuchana kwa Kihehe ni kudemula, hivyo mtoto huyo akaitwa Mdemu.
Watu wa ukoo wa Chavala, hasa akina Mdemu, huwa na si weusi huwa na rangi nyepesi na nywele nyekundu. Wanawake wa ukoo huu huitika kwa mwidikiso wa  Gogo. Sifa moja ya ukoo wa Chavala ni uganga wa kiasili.
Huyu mtoto mwingine wa Ndondole, yaani Kimamu, alizaa watoto wengi , lakini historia ya Uhehe  inawakumbuka sana  wawili Chota na Kindole .  Hawa walijulikana sana kwa uganga wa kuzindika nyumba, mashamba na hata nchi nzima. Kwa sababu hiyo waliitwa na watawala huku na kule kwenda kuwa zindika, hata Wakilwa waliokuwa wakitawala sehemu mbalimbali za Uheheni,  waliwaita ili wazindike nchi yao ili kusitokee tena kuingiliwa na maadui kama wale waliokuwa wakiteka watumwa au kushambuliwa tena na Vanyangologo.
Wakati mmoja  Chota na Kindole waliitwa  Lungemba ili wakatawale,  ili watu wawe na uhakika wa usalama. Chota aliyekuwa mkubwa akamwambia mdogo wake achukue ng’ombe na yeye achukue nchi. Kindole alikuja juu na kuanza kuchoma mikuki hovyo ng’ombe aliokuwa kakusanyiwa, huku akuisema ‘Sitaki ng’ombe nataka nchi’. Watu waliweza kuwatuliza na kumuomba Chota amuache mdogo wake atawale Lungemba na yeye akatawale Iwawa, nchi iliyokuwa na rutuba na wenyeji wake walikuwa tayari kumpokea awe mkuu wao. Chota akaafiki wazo lile.
Iwawa wakati huo ilikuwa ikitawaliwa na Munyaluwaho, mjukuu wa Mdongwe na Mkilwa wa ukoo wa Kavindikadodi. Mnyaluwaho aliposikia Chota anakuja akamuandalia karamu na kumpokea vizuri sana. Walipokula na kushiba na watu wakiendelea na sherehe ya kumpokea mkuu mpya, Chota, ambaye inasemekana alikuwamtu mwenye miraba minne, na alikuwa na ndevu ndefu za singa, alikuwa mweupe kiasi cha watu kumuita mwelu, alichukua mkuki na kumchoma nao Mnyaluwaho moyoni na kumuua palepale.  Wenyeji walitimka mbio hovyo,  ndugu wa Mnyaluwaho, akina Kavindikadodi wakakimbia kabisa nchi na kuhamia Udzungwa.  Hivyo Chota akaanza kutawala akiwa na uhakika hatapata upinzani kutoka kwa ndugu wa marehemu. Himaya ya Chota ilianzia Iwawa mpaka ilipo Iringa, na hata sehemu za Udongwe. Makao yake yakawa Luhota iliyokuwa katikati ya Udongwe.  Kuanzia wakati huo Wahehe walipata msemo ‘lusungu lwa Munyaluhwao’…yaani ukarimu wa Mnyaluhwao ulivyomponza….ili kuonya hatari za ukarimu kwa usiemjua vizuri….. Wahusika toeni maoni

 

 

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER