Pages

Saturday, August 6, 2022

MUFWIMI ALILAZIMIKA KUKIMBIA UHEHENI KUTOROKA KESI

 


Wawindaji walithaminiwa sana Uheheni kwani walikuwa chanzo cha mlo safi kwa jamii, hivyo sifa za Mufwimi zilitangulia kabla hajaingia Ng’uluhe. Alipofika Nguluhe akapokelewa vizuri na Mduda aliyekuwa mtawala wa eneo lile na kuwa mgeni rasmi wa Mutwa. Kila baada ya siku chache alikuwa akienda kuwinda na kurudi na nyama nyingi, Wahehe huita nyama hizi za porini  'mbelembo'. Kuna wakati alikuwa akipotea kwa siku kadhaa lakini hatimae akarudi tena, wenyeji wakampa jina la utani wakampa jina la Kayinguye.
Siku alizokuwa ametulia aliwafurahisha wenyeji kwa kupiga chombo chake cha muziki unachoweza kulinganisha na gitaa kilichokuwa kinaitwa Kimandinda, kilikuwa ni chombo cha muziki maarufu katika nchi ya Usagala wakati huo, nacho kama lilivyo gitaa kilikuwa na nyuzi sita.
Binti mkubwa wa Mduda alianza kumpenda Mufwimi, walianza kushinda pamoja jioni mpaka usiku mzito wakati watu wengine wamekwenda kulala, Mufwimi akimhadithia binti  yule habari zake  mbalimbali za kusisimua za maisha yake ya uwindaji. Haikuchukua muda mrefu ukaribu huo ukaanzisha mapenzi, siku moja Semduda, yaani binti ya Mduda akamwambia Muyinga kuwa anajihisi ana mimba. Mufwimi alijua kabisa kuwa kutakuwa na janga kubwa litakalomkumba pale  Mtemi Mduda atakapopata taarifa za mimba ya binti yake,  hivyo Mufwimi  akamwambia mpenzi wake kuwa kama atazaa mtoto wa kiume amfundishe kuwa mwiko wa ukoo wa Mombe ni Funo. Kisha akatoroka kuelekea kwao Ikombagulu.
Hakuna habari tena zinazosimuliwa kuhusu Mufwimi baada ya hapo, japo kuna habari zingine husema akina Mduda walimtafuta na kumuua Mufwimi kwa kosa la kumpa mimba dada yao bila ndoa,pengine hii ni hadithi tu kwani haijulikani kulikuwa na taratibu gani za kuishi  mtu na mzazi mwenzie zama hizo,
Mduda alimpa mjukuu wake jina la Mwamuyinga, yaani mtoto wa yule anayetangatanga. Mwamuyinga nae alikuwa na kuja kuwa muwindaji hodari kama baba yake, na pia alikuwa na busara sana, inaonekana alikuja kuwa kipenzi cha babu yake, hivyo alikuja kurithi sehemu ya utawala wa Babu yake, baada ya kifo cha Mduda.

Kuna hadithi za mapokeo kuhusu watawala waliokuja kumrithi Muyinga huyu wa kwanza, lakini nyingine ni wazi ni za kubuni, na pengine nyingine zimebadilika kutoka na kuwa zimekuwa zikirithiwa kwa kuhadithiana. Kilicho wazi ni kuwa kwa vyovyote Muyinga hakuweko kabla ya mwaka 1760, hivyo kutaja majina mengi ya warithi wa Muyinga wa kwanza na kudai kuwa wengine walitawala mpaka uzee sana  kunakosa mashiko kutokana ma  muda. 
Huwa majina kama Kitova, Lalika,  Mdegela, Kilonge hutajwa katika orodha ya watawala warithi wa Muyinga, lakini kuna wenye kudhani kuwa Kitowa ni jina jingine tu la Muyinga wa kwanza, na Lalika ni jina la mdogo wake Mdegela aliyekuwa babu mzazi wa Mkwava. Kuna wanaosema Kitoa na Mdegela ni jina lamtu huyohuyo mmoja, wengine husema Mdegela alikuwa mtoto wa Kilonge, na wengine husema Kilonge alikuwa mtoto wa Mdegela, na huo ndio mchanganyiko wenyewe. Kwa kuendeleza historia tukubali kuwa Kilonge alikuwa mtoto wa Mdegela.
Inasemekana kuwa akina Muyinga walikuwa wakioa katika ukoo wa  Mveyange, Kindole na Vanyamahuvi. Mpango huu ulikuwa tofali moja katika ujenzi wa kabila moja la Wahehe..
Kilonge alimuoa binti mmoja wa Kindole, ukumbuke kuwa Kindole alikuwa mtawala wa Lungemba baada ya msuguano na kaka yake Chota, hivyo baada ya Kilonge kumuoa Sekindole, binti huyo alipewa na baba yake askari 200 wa kumsindikiza na kumlinda na hatimae wawe walinzi wa sehemu aliyotawala Kilonge. Labda niongeze neno hapa, Wahehe walikuwa na utaratibu wa kuwa na vikosi vya askari mia mbili mia mbili. Baada ya kukabidhiwa  jeshi hili na mkwewe,  Kilonge akaanza kutamani  kutawala Nguluhe yote kama ilivyokuwa enzi za Mduda, hivyo akamtimua kaka yake aliyeitwa  Manga, ambae akalazimika  kukimbia na wafuasi wake ambamo pia walikuweko Watemikwila.
Kundi hili lilikimbia mpaka nyanda za juu za Ubena, sehemu ambayo sasa inaitwa Masagati. Jina hili lilitokana Mwarabu mmoja aliyeanzisha shamba la miti ya mpira na kuamua kupaita mahala hapo Muscat akikumbuka nchi aliyotoka, ugumu wa matamshi  ya jina hilo ukapafanya hapo paitwe MASAGATI. .   

No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER