Pages

Wednesday, August 3, 2022

UNAJUA CHANZO CHA JINA MTAGE?

 


Kamwene vanyalukolo, leo naomba niendelee kutaja makundi mengine makubwa ya watu walioingia Uheheni. Kundi la kwanza ni lile lililotokea  Ukimbu, hili kundi linadhaniwa liliingia wakati mmoja na Wakilwa. Kundi hili lilikuwa likijiita Vanyandembwe, ndembwe ni tembo, na Vanyandembwe walikuwa wakidai asili yao ni tembo.
Kwa nyakati hizi ni ukoo wa akina Ugulumu na Ifweni ndio wajukuu wa kundi hili la Vanyandembwe. Baadae sana liliingia kundi jingine kutoka Ukimbu hili liliongozwa na  Mufilinge aliyekuwa mtoto wa Musawila aliyekuwa mtawala wa Ukimbu wakati huo. Na kwa sababu hiyo ukoo wa Mfilinge huitwa Vasawila, wao walikuja kuishi sehemu za kutoka  Makungu mpaka jirani ya Wasa na eneo hilo lilikuja julikana kama Usawila.
 Inawezekana walikuwa na uhusiano na Vanyamahuvi kwani , walipofika Uheheni walikaribishwa na Vanyamahuvi na kupewa eneo la  Makungu watawale, lakini baada ya muda mfupi waliongezeka na kutawala kuanzia Kiponzelo mpaka Malangali, jambo lililowaletea uadui na ukoo wa Nyilowa na Nyakunga ambao hatimae walihamia Uhafiwa na Udongwe.
Hawa Wasawila walipoingia uheheni walikuwa wakivaa aina ya nguo iliyotengenezwa kwa magamba ya miti yaliyotwangwa,  wenyeji wakawaita Vanyamwenda.
Pia walikuwa waganga wazuri hivyo wanawake zao wakapewa mwidiko ( muitikio) wa Ganga, wakati wanaume zao waliitika kwa Mikwile au Nyasite.
Wasawila waliendelea kukumbusha kuwa wao ni Wakimbu. Makundi mengine yalichukua lugha ya wenyeji na hakika Kihehe kilipata mchango wa maneno kutoka lugha nyingi za wageni walioingia.
Kwa mfano Wakimbu ndio walioleta neno Mtemi,  ambalo walilikopa ktoka kwa jirani zao Wanyamwezi. Wahehe wakaanza kutumia neno Wutemaa kumaananisha utawala, kabla ya hapo walikuwa wakitumia neno Wumutwa ambalo lilitoka kwa Wabena.
Kwa Wahehe jina Mtemi hutumika likiwa na maana mkata shauri au hakimu, kutema ni kukata. Wahehe waliamini mtunga sheria asiyehukumu na kuadhibu hawezi kuheshimiwa.
Lugha ya Kihehe imebadilika sana, kwa mfano ,nakumbuka wimbo ambao babu yangu alinifundisha na kunambia kuwa ulikuwa wimbo wa askari wa Kihehe walipotoka vitani, wacha niuimbe mwenye kuweza kuutafsiri tafadhali fanya hivyo kwenye sanduku la Comment hapo chini;
 Mitela kimalimali na manyile mtalavande
Oh Likalikasela 
Oh likoko ngomba mitela

Ukoo wa Ndondole hasa akina Kindole walisifika kupenda kujikweza kuwa wao ni ukoo wenye hadhi,  wanaume walijiita Mulugu Mutavangu, maana yake kiongozi wa wapiganaji na wanawake wakajiita Vanyatage yaani waliotupwa, hii ilikuwa kukumbusha kitendo cha Kindole kung’ang’ania kutawala Lungemba, na kumtupa kaka yake Chota aliyekwenda kutawala kwa Mnyaluhwao.
Baadae Wahehe waliendeleza utamaduni huu kwa kumuita mwanaume  mwenye hadhi Mulugu na mwanamke mwenye hadhi Mtage.

2 comments:

  1. ino ya mtage ulonzile pi mtwa vangu ve

    ReplyDelete
  2. Nyee nahangaika kupata historia nakuandikia na kukusomea nikusomee?

    ReplyDelete

STAT COUNTER