Pages

Sunday, April 4, 2010

Consolata Primary School

Barabara Mbili
Jiwe la adhabu nje ya shule ya Chemchem
Katika kipindi nilipokuwa nasoma, Consolata aka Chemchem, eneo lote linaloitwa Frelimo lilikuwa pori tu, palikuwa na njia ya mkato toka hapo shuleni mpaka Makorongoni. Nilikuwa nikiishi Barabara Mbili kwenye nyumba ambayo kwa sasa ni kilabu cha pombe. Wakati huo kulikuwa na wenzetu wanakaa Nduli ambao nao walikuwa wanawahi kila siku kuja shule asubuhi saa moja na nusu.Ukichelewa prefect alikuwa anaandika majina, prefect mmoja ambaye sasa ni mkuu fulani, alikuwa bingwa wa kupokea hongo yamatunda kama mitoo, misasati, na mifudu na mahindi ya kuchoma ili asikuandike jina ikiwa umechelewa. Moja ya adhabu mbaya ilikuwa ni kupewa nyundo na kuligonga jiwe lililopo kwenye uwanja wa shule, mwalimu alitakiwa awe anasikia akiwa darasani, kwa kawaida baada ya kugonga dakika kumi ilikuwa kama unajigonga ndani ya kichwa. Kati ya starehe za wakati huo ilikuwa ni kuogelea katika kisima kilichokuwa kwenye makutano ya barabara itokayo stendi na ile iendayo Ilala, wakati huo hapo ilipo stendi palikuwa ni makaburi tu. Starehe nyingine ilikuwa ni kutengeza bunduki zilizoitwa Nyongamembe, au kuteremka Ruaha kwa ajili ya kuchuma mitoo,misasati na mifudu na kuogelea kuvua samaki na kutengeneza kamba za katani kwa kuzileta shule kwenye kipindi cha Maarifa ya Nyumbani. Adhabu ya kufungiwa darasa zima kutokwenda kula mchana nayo ilikuwa maarufu sana.
Nakumbuka hapo mtaani barabara mbili tulianzisha bendi kama zile za shule kwa kuwamba ngoma sisi wenyewe. Ila tuliwahi kuibiwa ngozi na mwalimu mmoja wa shule ya chini ya mti ambaye wote tulikuwa tunamuogopa kwani aliwahi kujaribu kujinyonga chooni kamba ikakatika akawa kama zezeta fulani lakini hiyo shule ya chini ya mti imekuwa shule maarufu mpaka leo.

1 comment:

  1. unamkumbuka marehem mwalimu ngalawa!alikuwa chemchem!

    ReplyDelete

STAT COUNTER