Pages

Saturday, July 30, 2022

UNAJUA WAHEHE WALITOKEA WAPI 2 ? marekebisho

 


Wabena ndio chanzo cha Wahehe. Inasemekana jina la kabila hili lilitokana na kutofautiana katika mshangao na kabila lao mama la Wabena. Wahehe walikuwa wakishangaa kwa kusema He he, Wabena walikuwa wakishangaa kwa kusema khe khe. Baadaye Wahehe walitumia sauti hiyo hata wakati wakiwa vitani. Kama nilivyosema katika sehemu ya kwanza ya simulizi hii, makundi mawili ya wabena yaliondoka Nyumbanitu na kuelekea Kaskazini mashariki na kuja  kuishi kwa muda Magharibi mwa ilipo Malangali sasa.  Lakini tena kukaweko na mgawanyiko, kundi moja lilielekea  bonde la Lyambangali na kuanzisha  kabila la Wasangu , wakati kundi jingine likielekea upande wa pili na hili likaja kuwa chanzo cha Wahehe. Katika kugawanyika huku, sehemu waliyoanzia kugawanyika ikaitwa  Igawilo maana yake penye kugawa nchi. 

Kama ilivyokuwa katika tabia za Kibantu watu hawa waliokuja kuitwa Wahehe awali waligawanyika katika koo mbalimbali, japo inasemekana walikwisha anza kujitambulisha kama Wahehe.  Kati ya  koo  maarufu walikuweko  akina;  
Vigawilo – Hawa ni wale waliobaki pale Igawilo,   na baadae wengine wakaaza kusambaa katika bonde la Lyandembela na kuanza kuitwa Vilongo. Mwiko wao hawa ulikuwa bandama, jamaa wa ukoo huu ni akina Kibodya na Mugandu.
Vahafiwa – hawa walienea katika sehemu zinazoitwa siku hizi Tanangozi, welu, kalenga Ntsihi, na maeneo yanayozunguka mji wa Iringa.

Kuna wakati maeneo haya yalipata uhaba mkubwa wa mvua hivyo kukawa na njaa na hata watu wengi  wakafa kwa njaa, waliosalimika walikuja kupata mwidikiso wa  Vahafiwa maana yake waliofiwa na wengine walikuwa na mwidikiso wa Mponela yaani aliyepona njaa. 

Wengine walikuja kuitwa Vanyalugome kwa sababu ya desturi yao ya kutengeneza mitego ya wanyama kwa  kuchimba mahandaki.

Mwiko wao hawa ilikuwa ni nyopolwa, Yaani mimba ya mnyama yoyote.

Labda niseme hapa hapa kuwa mwiko maana yake hawaruhusiwi kamwe hata kuonja nyama hiyo.

Kati ya koo zinazojulikana kutoka kundi hili ni akina Mugovano, Mukemangwa na mutono,

Vanyandevelwa- maana yake wepesi kuchokozwa, makazi ya kundi hili yalikuwa kati ya barabara mbili zilizoanzia Iringa, yaani ile ya kwenda  Dar es Salaam na ile ya kwenda Dodoma

.Awali nao mwiko wao ulikuwa nyopolwa lakini walikuja kunyangwa nchi na kundi lililoitwa Vanyamahuvi na kuja kutawaliwa nao.

 Hawa Wanyamahuvi wakaja kutwaa jina la Vanyandevela lakini wakaendeleza mwiko wao ambao ni ndege kanga, Ni vigumu siku hizi kupambanua nani ni Mnyandevela wa awali na nani Mnyamahuvi wa awali

Vategeta hawa walikuwa na umuhimu sana katika kabila la wahehe kwani walikuwa mafundi wa kufua chuma.

Wategeta ndio waliounda mikuki, mundu shoka na kadhalika. Wategeta waliishi karibu na kila ukoo wa Wahehe na hasa sehemu zenye mchanga uliweza kutoa chuma, wengi walikuwa warefu wenye maungo yenye afya na hivyo basi waliweza kufikia kutawala katika sehemu nyingi walizokuwa wakiishi.

Wategeta waligawana kazi, walikuwa na sifa ya kuwa wana mipangilio katika maisha yao.  Wale waliokuwa mabingwa wakutafuta kuni kwa ajili ya mkaa wa kuyeyushia chuma waliitwa Vanyantsagala …nzagala ni kuni, baadae walikuja kufupishwa na kuitwa Wasagala.

 Wategeta ambao walikuwa na utaalamu wa kuchagua mchanga bora kwa chuma waliitwa Vayunga, ambao ndio chanzo cha Watsungwa. Kutokana  majina haya walipoenea na kuwa wengi sehemu waliyoenea Vayunga ikaitwa Utsungwa na walikoenea Wasagala ikaitwa Usagala.

 Mwiko wa Wategeta ni mato kwa Kiswahili mbawala na wengine mwiko wao ni dundulu yaani twiga. Inasemekana waliamini kuwa kwa kula nyama ya wanyama hao  wangepata ukoma ,kwani ngozi ya binadamu huwa na mabaka meupe kama twiga, kama ameambukizwa ukoma.

Kati ya koo za Wategeta maarufu ni Chusi na kina Mveyange

Wakilwa,,, hawa waliitwa hivi kwa kuwa walitokewa Kilwa na kuingia sehemu inayoitwa siku hizi Mufindi kwenye robo ya kwanza  ya karne ya 16. Yaani mwaka 1500. Hawa hawakutokana na Wabena kama Wahehe wengine.

Hawa walikuwa na ngozi ya maji ya kunde na walikuwa na nywele nyingi mikononi na kifuani.  Nywele ambazo Wahehe huziita Lyagi,hivyo Wakilwa pia wakaaitwa Vanyalyagi. Dalili hizi ziliwatofautisha na wabantu wengine. Inasemekana walipokuwa badi Kilwa, walichanganyika na Wareno na Washirazi waliokuwa tayari wametua Kilwa wakati huo.

Kati ya Wakilwa wa Uheheni ni akina Kihwele ambao walipoenea Uheheni walionyesha kutengeneza vifaa vya chuma bora kuliko Wategeta.  Huko Katanga Kongo kuna ukoo unaitwa Kiwele, na kuna uwezekano kuwa ni ndugu wa Kihwele wa Uheheni kwani wote walikuwa wakizika wafu wao kichwa kikielekea mashariki, kwa kukumbuka kwao  Kilwa, ambayo iko mashariki mwa Katanga na Uhehe pia,


No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER