Pages

Wednesday, July 27, 2022

HIVI UNAJUA WAHEHE WALITOKEA WAPI? FUATILIA HAPA

Isimila

 Tukirudi nyuma kama miaka 11,000 iliyopita tuna ushahidi kuwa walikuweko binadamu ambao walitumia silaha za kuchonga mawe, kihistoria zama hizo hujulikana  kama zama za mawe au stone age era.

 Kilomita chache kutoka mji wa Iringa, ukiwa unaelekea  na barabara kuu iendayo Mbeya, kuna sehemu inaitwa Isimila,

hapa katika bonde moja kubwa kunapatikana ushahidi wa vipande vya mawe vilivyochongwa kwa ajili ya kazi mbalimbali hasa za uwindaji katika zama hizo.

Wahehe walipopafahamu hapa ndipo wakapaita Isimila, jina linalotokana na neno la Kihehe ‘simo’, maana yake fumbo. Kwani kuweko kwa silaha zile za mawe kwa wahehe lilikuwa fumbo.

Ukiingia sehemu za Usagala kuna mlima uitwao Ikombagulu, huku kuna pango ambako iko michoro ya zamani sana, kuonyesha kuwa pia kulikuwa na watu waliokuwa na utamaduni wa michoro ya mapangoni.

Katika bhonde la mto Lya Ndembela kuna ushahidi wa kuishi watu ambao Wahehe katika simulizi zao waliwaitwa Vanyidaha,

 watu hawa waliacha ushahidi wa utamaduni uliofanana sana na utamaduni wa Wairaki wa huko Mbulu, kuna watafiti wanasema wakazi hao walikuwa Wairaki wa zamani.

 Baadhi ya utamaduni waliouacha Wairak hawa ni kulima kando ya mito maarufu kwa jina la finyungu, na kutumia mawe ya kutoka mtoni kusagia nafaka.  Wahehe waliendeleza utamaduni huu na huita mawe hayo nunulilo.

Pia walikuwa na utamaduni wa kujenga majengo ya mviringo kutumia mawe,mpaka miaka ya mwanzoni ya 60 kulikuwa na mabaki ya jengo la namna hiyo kule Kiwiluka, ambalo lilikuja fumuliwa taratibu na watoto. Kule Engaruka, Monduli kulikuwa na mabaki ya majengo ya aina hiyohiyo.

Katika bonde hilo la Lyambangali kulikuwa na masalia ya majengo mengine, yaliyojengwa kwa matofali ya kuchomwa. Wahehe katika simulizi zao za kale walisema waliojenga nyumba hizo walikuwa Waiyenzele,

 Ugogoni kulikuwa na masalia ya majengo kama hayo na Wagogo walisimulia kuwa wajenzi wa magofu yale walikuwa Wamankala, lakini hakuna maelezo zaidi kuhusu watu hawa kuwa Waiyenzele au Wamankala walikuwa wa aina gani , walitoka wapi, na walienda wapi.

Watu wengine waliokuweko katika nchi hii walikuwa ni Mbilikimo. Kuna hadithi za kale za Wahehe kuwa hawa Mbilikimo walikuwa hodari kwa mishale, kwa vile walikuwa wafupi walikuwa wanawaona watu wengine mapema na kupiga kelele ‘Ngulenge’ yaani  nimekwisha kulenga.

Kama mtu alimuona Mbilikimo kwanza alimwambia , Nguwene’  maana yake nimekuona, na hawa mbilikimo, walikuwa    wakiuliza  umbonie kwi? Kwa sababu hiyo mpaka zama hizi Mbilikimo au watu wafupi Uheheni, hujulikana kwa jina la utani, Mwanangulenge au Wambonie kwi

Kundi jingine la watu waliokuweko katika uwanda huu wa Wahehe kabla ya ujio wa Wahehe walikuwa Wahamya au kwa Kiingereza huitwa Bushmen, hawa ni wafupi lakini si wafupi kama mbilikimo na pia huwa ni weupe kiasi.

Hawa walifika mpaka sehemu za Manyoni na kuanza kuchanganyika na wenyeji, wajukuu za Wahamya hawa waliobakia Uheheni huitwa kwa mwidikiso wa Mkemwa na mwiko wao (msilo), ni nyama ya pundamilia.

Ukoo wa kina Mwisaka chanzo chao ni Wahamya hawa.

Kundi la mwisho ni Vahumma, Wahehe hutamka Vahumba, ni kundi ambalo kwa  Kiingereza hujulikana kama Hamitic.

Hawa nao walienda kuweka maskani yao katika bonde la Lyambangali .


No comments:

Post a Comment

STAT COUNTER